23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Japan yatoa mabilioni kusaidia miradi ya halmashauri

LEONARD MANG’OHA-DAR ES SALAAM

UBALOZI wa Japan umetoa msaada wa zaidi ya Sh bilioni 1.374 kusaidia ujenzi wa miradi saba ya elimu na afya katika halmashauri mbalimbali nchini.

Akizungumza Dar es Salaam jana katika hafla ya utiaji saini mikataba ya utekelezaji wa miradi hiyo, Balozi wa Japan hapa nchini, Shinichi Goto, alisema miradi itakayotekelezwa kupitia fedha hizo ni pamoja na ujenzi wa maabara ya sayansi katika Shule ya Sekondari ya Kassim Majaliwa ya Ruangwa mkoani Lindi itakayogharimu Sh milioni 195.

Pia alisema katika kukuza uchumi wa viwanda, Serikali ya Tanzania inaweka mkazo katika elimu ya sayansi hasa ujenzi wa maabara katika shule za sekondari.

“Katika Wilaya ya Ruangwa, kati ya shule za sekondari 16 ni shule tatu tu ndizo zina maabara. Kwa sasa wanafunzi wa Shule ya Sekondari ya Kassim Majaliwa haina vifaa na maabara za masomo ya sayansi,” alisema Goto.

Miradi mingine ni pamoja na ujenzi wa uboreshaji wa mazingira ya elimu wilayani Chato mkoani Geita ikiwamo ujenzi wa vyumba vya madarasa, vyoo na ununuzi wa samani katika shule za msingi za Idoselo na Nyambogo utakaogharimu Sh milioni 196, ujenzi wa Zahanati ya Batibu katika Halmashauri ya Ushetu wilayani Kahama, ujenzi utakaogharimu Sh milioni 215 na kupunguza adha kwa wananchi wanaolazimika kutembea umbali wa kilomita 12 kufuata huduma za afya.

Pia utahusisha ujenzi wa wodi ya wazazi katika Hospitali ya Wilaya ya Maswa mkoani Simiyu utakaogharimu Sh milioni 195, ujenzi wa zahanati, nyumba ya muuguzi na choo na ununuzi wa samani katika Zahanati ya Mafumbo wilayani Muleba utakaogharimu Sh milioni 194.

“Mradi wa sita ni wa ujenzi wa madarasa katika Shule ya Sekondari ya Sokoni II Wilaya ya Arumeru mkoani Arusha. Shule hii ilianzishwa mwaka 2015 ili kupunguza ugumu kwa wanafunzi kwenda shule za mbali katika kata nyingine, Serikali ya Japan imeamua kutoa shilingi milioni 195 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa na kununua samani.

“Mradi wa tano ni wa ujenzi wa hosteli katika Sekondari ya Kabasa katika Wilaya ya Mji wa Bunda mkoani Mara.

Shule hii haina hosteli ya wanafunzi. Kwa sababu hiyo wanafunzi wengi inawabidi watembee umbali mrefu kufika shuleni na hili linaathiri maendeleo yao ya kimasomo darasani,” alisema Goto.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles