30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Janet Otieno azitazama tuzo za Afrima Ghana

NAIROBI,KENYA

MIONGONI mwa waimbaji Gospo wanaofanya vizuri katika ukanda huu wa Afrika Mashariki ni Janet Otieno kutoka nchini Kenya, kupitia nyimbo zake Asante, Nifunze, Niwezeshe, Uniongoze na Roho Wako zenye mguso wa kipekee.

Hivi karibu jijini Dar es Salaam Juma3tata lilipata nafasi ya kukutana na mwimbaji huyu nyota wa Gospo na kufanya mazungumzo yafuatayo ikiwa ni siku chache toka arudi Afrika akitokea nchini Canada alipokwenda kufanya ziara ya kimuziki, karibu.

Juma3tata: Mapokezi ya muziki yako yalikuwa vipi kule Canada?

Janet: Nashukuru huduma yangu imekua, nilikuwa nafanya ziara katika makanisa na maonyesho machache, mapokezi yalikuwa mazuri tofauti na matarajia, Mungu ni mwema sana.

Juma3tata: Mungu amekupa nafasi ya kuzunguka sehemu mbalimbali duniani, je unaweza kuwaambia mashabiki zako historia yako kwa ufupi ili wafahamu ulipotokea?

Janet: Nimeanza kuimba nikiwa mdogo mpaka sasa nashukuru naendelea vizuri, mimi huwa nasema mafanikio ni vile kutoa nyimbo zikawagusa watu, zikamtoa mtu sehemu moja na kumpeleka sehemu nyingine nzuri.

Juma3tata: Vipi kuhusu familia yako inaunga mkono unachokifanya na unagawa vipi muda wako?

Janet: Familia ipo na mimi katika kila hatua ninayopiga, nimeolewa na nina watoto watatu, wa kike wawili na wa kiume mmoja, changamoto ya muda ilikuwa mwanzoni lakini sasa hivi nikiaga nakwenda kwenye huduma napata baraka kutoka nyumbani.

Juma3tata: Ukiwa mapumzikoni unapenda kufanya shughuli gani?

Janet: Huwa napenda sana kupika ili kubadilisha ‘diet’ mara nyingi napenda kupika mashed potato (viazi vya kusagwa), chicken au fish au beef stew (rosti ya kuku, samaki au nyama ya ng’ombe).

Juma3tata:Umekuwa ukitoa nyimbo kwa muda mrefu je huna mpango ya kuachia albamu?

Janet: Natarajia kutoa albamu mwishoni mwa mwaka huu Mungu akijaalia lakini mwanani natarajia kutembelea Tanzania kwa sababu kuna watu wanasapoti muziki wangu.

Juma3tata: Hapa Tanzania kuna waimbaji wengi wazuri, ni mwimbaji yupi anakuvutia zaidi?

Janet: Itakuwa ngumu kuwataja wote kama ulivyosema wengi wanafanya vizuri kazi ya Mungu, kwa uchache Christina Shusho niliwahi kufanya naye wimbo, Angel Benard, Goodluck Gozbert, Joel Lwaga,Paul Clement, Walter Chilambo na wengineo ambao siwezi kuwataja wote nikisikiliza nyimbo zao zinanibariki.

Juma3tata: Katika ziara uliyoifanya Canada nini ulijifunza na kuna ziara ya hivi karibuni?

Janet: Nimejifunza kuwa Mungu ni mwaminifu anayeweza kumheshimisha kila mmoja wetu. Mambo yakikaa sawa basi wiki hii natarajia kusafiri tena kwenda nchini Marekani, nitakaa huko kwa wiki mbili sababu natakiwa kurudi Kenya kisha niende Ghana kwenye tuzo za Afrima kwa sababu walinipa mwaliko na wakasema itapendeza nikiwepo siku ya tuzo kuanzia Novemba.

Juma3tata: Ulipata vipi nafasi ya kushiriki kwenye tuzo hizo ambazo mwaka huu wapo wasanii wetu Ali Kiba, Diamond Platnumz, Vanessa Mdee na Maua Sama ndiyo wapo kwenye tuzo hizo?

Janet: Nimeingia kwenye tuzo nikiwania kipengele cha Msanii Bora wa Kike katika muziki wa kuhamasisha (Best Female Artiste In African Inspirational Music), ninaomba watanzania waingie katika ukurasa wangu wa Instagram @janetotieno watakutana na linki inayoelekeza namna ya kunipigia kura au tovuti yao www.afrima.org.

Juma3tata: Asante kwa muda wako

Janet: Shukrani, nimebarikiwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles