28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Jaji Ramadhan astaafu Mahakama ya Afrika

Jaji Augustino RamadhaniNa ELIYA MBONEA – ARUSHA

RAIS wa Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu (AfCPHR), Jaji Augustino Ramadhani, amestaafu utumishi katika mahakama hiyo, huku akijivunia mafanikio ya kutafsiri maelezo muhimu ya mahakama hiyo kwa lugha adhimu ya Kiswahili.

Jaji Ramadhani aliapishwa kuwa Jaji wa Mahakama ya Afrika mwaka 2010 baada ya kustaafu nafasi yake ya Jaji Mkuu wa Tanzania na mwaka 2014 alichaguliwa kuwa rais wa taasisi hiyo na kufanikiwa kuitumikia kwa miaka sita.

Akizungumza katika viwanja vya mahakama hiyo mjini hapa jana baada ya kumwapisha Jaji Marie-Therese Mukamulisa kutoka Rwanda na Jaji Ntyam Ondo Mengue kutoka Cameron, Jaji Ramadhani alisema anajivunia mafanikio aliyoyapata na kuomba maelezo hayo muhimu ya lugha ya Kiswahili kuanza kutumika.

Alisema kuingia kwa lugha adhimu ya Kiswahili ni mafanikio makubwa kutokana na ukweli kuwa wakati alipokuwa akiingia kushika wadhifa wa rais wa mahakama hiyo alikuta maelezo hayo yakiwa yamewekwa kwa lugha mbili tu – ya Kifaransa na Kiingereza.

“Mafanikio haya ni makubwa kwani tumeweza kutafsiri maelezo muhimu ya Mahakama ya Afrika kwa Kiswahili. Haya ni mafanikio makubwa kwetu, hasa Tanzania tukiwa ndio wenye lugha yenyewe ya Kiswahili.

“Kilichobakia sasa ni kianze kutumiwa tu kwani tayari Rais Mstaafu Jakaya Kikwete alishazindua maelezo hayo mwishoni mwa mwaka jana,” alisema Jaji Ramadhani aliyewahi kuchukua fomu ya kugombea urais kupitia CCM mwaka 2015.

Jaji Ramadhani alisema mbali na kufanikiwa kukiingiza Kiswahili, pia lugha Kiarabu inayoongoza katika Bara la Afrika kwa kuzungumzwa na watu nayo iliingizwa katika maelezo hayo muhimu ya mahakama.

Akielezea kuhusu nafasi ya Tanzania tena kushika wadhifa huo wa Rais wa Mahakama ya Afrika, Jaji Ramadhani ambaye ni Mchungaji wa Kanisa la Anglikana Zanzibar, alisema fursa hiyo itakuwa wazi ifikapo mwaka 2018 endapo kutakuwa na Jaji atakayehitaji kugombea.     

Alisema Bara la Afrika katika utoaji wa majaji wa mahakama hiyo lilijigawaa katika kanda tano ambazo ni Kanda ya Afrika Kaskazini, Kusini, Mashariki, Magharibi na Kanda ya Kati ambapo kila ukanda hutoa majaji wawili.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles