31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Jaji Chade: Mahakama izingatie utawala wa sheria

KULWA MZEE -DAR ES SALAAM

JAJI Mkuu mstaafu, Mohamed Othman Chande, ameacha wosia mzito kwa mahakama, akitaka kuzingatiwa utawala wa sheria, kuheshimu Katiba na uhuru wa mahakama  ambao kwa kiasi kikubwa umekuwa ukilindwa.

Alisema hayo wakati wa hafla ya kuagwa kitaaluma, iliyofanyika ukumbi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Dar es Salaam jana.

Jaji Chande alisema uhuru wa mahakama sio kitu kama jiwe, uhuru wake unatakiwa ulindwe, utetewe na watu waelezwe, ikiwamo taasisi nyingine zinazoupima.

“Katika mambo mengi niliyozungumza, mojawapo ni kupeana wosia kuhusu suala la utawala wa sheria, kuheshimu Katiba na uhuru wa mahakama.

“Kwa kiasi kikubwa mahakama yenyewe inalinda uhuru wake, Katiba, sheria zinajitosheleza kulinda uhuru wa mahakama, mahakama sio kama jiwe kwani uhuru wake inabidi utetewe, ulindwe na watu waelezwe,” alisema Jaji Chande.

Alisema katika utawala wake, mageuzi makubwa yamefanyika na yanaendelea kufanyika, ikiwemo kutenganisha majukumu ya wasajili wa mahakama na watendaji wake, mfumo mpya wa usikilizwaji wa malalamiko ambapo asilimia 98 yanasikilizwa kwa mwaka na kwisha.

“Mengi yalianzishwa, mengine kabla yangu na mengine niliyaanzisha, kila jaji mkuu anaweza kuanzisha mambo mapya. Ushirikiano mkubwa unaendelea.

“Mimi mpaka sasa hivi, Rais aliniteua kuwa Mwenyekiti wa Baraza la Chuo Kikuu cha Sokoine katika suala la utawala bora. Mahakama pia wananialika katika mafunzo ya majaji wapya, tunafundisha na kutoa michango yetu,” alisema.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma, alisema utaratibu wa kuagana kitaaluma ni wakati wa kutathmini tangu alipotoka chuo kikuu miaka 45 iliyopita hadi alipostaafu mwaka 2017.

Profesa Juma alisema katika utawala wake, Jaji Chande ameyashuhudia mabadiliko na hivyo tunatathmini mambo yake mengi, ikiwemo utaratibu wa mahakama kujitawala kimkakati, ikiwa ni pamoja na kupeleka haki maeneo ambayo hayajafikiwa, mfano kupeleka mahakama za mwanzo katika tarafa kwa wananchi.

Alisema wananchi wengi hawapati haki sababu kuna mahali mahakama hazijafika.

“Mfano haki za binadamu mtetezi ni wewe mwenyewe, ukikosewa unaenda mahakamani kama Mahakama haiko karibu utetezi wako unakuwa ngumu,” alisema.

Jaji Profesa Juma alisema hakuna muhimili unaofanya kazi kwa uwazi kama mahakama, nafasi ya kuingiliwa ni ngumu, labda kwa utashi wake, watu waendelee kuwaamini, wawapime kwa majukumu yao na kama hawajaridhika wakate rufaa.

Akizungumzia suala la rushwa, alisema lipo kila mahali, hata katika ripoti ya Jaji Warioba lilizungumziwa,  na kwamba mahakama inalizungumzia na kulikemea ikiwa ni pamoja na kumpa kitambulisho kila mtumishi wa mahakama.

“Watumishi wa mahakama wana vitambulisho na majina, hivyo akiomba rushwa ni yeye si watu wote, niwaombe na wananchi ukiombwa rushwa useme na uwe tayari kutoa ushahidi, nenda mpaka Takukuru mtaje mla rushwa.

“Tunawasaidia wananchi wasiingie kwenye mitego ya rushwa, tunawaelimisha waelewe taratibu za mahakamani,” alisema.

Waziri Mkuu mstaafu, Mizengo Pinda akimzungumzia Jaji Chande, alisema wameshirikiana sana katika kuleta mabadiliko ndani ya mahakama.

“Nilimwambia alipoteuliwa kuwa Jaji Mkuu kwamba huko ni kugumu, ahakikishe rushwa hainuki kwani ikiingia itaharibu mfumo mzima, kweli alijitahidi kufanya kazi awezavyo, kwa sisi tunaomjua, tunajua kafanya mengi.

“Kajitahidi kuhakikisha kesi zilizorundikana zinapungua, kajituma kufanya kazi, namna alivyosimamia na kudhibiti rushwa katika mahakama,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles