24.5 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

INNOCENT V HOPE WA MAREKANI HUMWAMBII KITU KWA SHUSHO, MARTHA BARAKA

 SWAGGAZ RIPOTA 

MIONGONI mwa wanamuziki wa Gospo wenye asili ya Afrika kutoka nchini Burundi wanaokuja kwa kasi huko Kentucky, Marekani ni Innocent Vyizigiro Hope (Innocent V Hope). 

Hivi karibuni jarida hili la Swaggaz, lilikutana na Innocent na kupiga naye mastori kibao kuhusu muziki na maisha yake ya kawaida akiwa kwenye mpango wa kuachia ngoma yake, Neema Bado Ipo. 

Swaggaz: Innocent V Hope ni nani na ilikuwa vipi ukaingia kwenye sanaa ya muziki? 

Innocent: Mimi nimeanza kuimba nikiwa mtoto mdogo kwenye ‘Sunday School’ nikiwa nafuata mwongozo wa baba na mama yangu ambao walikuwa viongozi wa kwaya. 

Nilipokua nikajiunga na kwaya ya wakubwa mpaka nikaanza kujifunza mambo ya muziki kama kupiga ngoma, kinanda na gitaa zote za solo na base, napiga kiasi kwamba naweza kutengeneza biti kwenye kinanda. 

Nilitoka Afrika na kuja hapa Marekani mwaka 2015 nikaendelea kuimba kwenye kwaya na Mungu akaendelea kunitendea maajabu kwenye kipaji changu mpaka mwaka jana nilipoamua kuwa mwimbaji binafsi. 

Nilikuwa na shauku ya kurekodi ngoma zangu mwenyewe na 

 nilikuwa nimepanga niutoe mwonzoni mwa mwaka huu ila kwa sababu ya corona ikabidi niutoe mwezi huu wa saba na sasa nimeingia rasmi kwenye muziki naomba mashabiki wanipokee. 

Swaggaz: Changamoto zipi unakutana nazo kwenye muziki wako hapo Marekani? 

Innocent: Changamoto zipo nyingi, mwanzoni kabla sijaamua kutoa wimbo wangu binafsi nilikuwa naimba nyimbo za waimbaji mbalimbali na kuposti kwenye mtandao na kama unavyojua sio kila mtu atakufurahia, wengine watakuponda watakwambia hufanyi vizuri. 

Lakini Mungu alinisaidia nikapata washauri wazuri kama vile Maisha Mtoto wa Manase akaniamba wanadamu wataendelea kuongea ila kazana na ujue unafanya nini na nikakumbuka maneno ya Christina Shusho aliwahi kusema ukishajua unachofanya wanadamu hawawezi kukuyumbisha. 

Swaggaz: Ukiwa kama mwimbaji mpya unayetamani muziki wako usikike Afrika Mashariki, ni waimbaji gani unatamani kufanya nao kazi? 

Innocent: Naomba Mungu anifanyie njia siku moja nije nifanye kazi na Christina Shusho, Bonny Mwaitege na Martha Baraka. Kuna wengi ila baadhi ni hao kwa sababu nilikuwa nawasikiliza tangu nikiwa mdogo na huwa ninawaangalia wanachofanya na nyimbo zao zote naweza kuziimba, nazipenda na zimenishawishi niingie kwenye tasnia hiyo na huku Marekani wapo kuna Maisha Manase na Joshua Promise. 

Swaggaz: Unajiandaa kutoa audio na video ya wimbo wako mpya, Neema Bado Ipo, ni ujumbe gani unataka uwafikie mashabiki zako? 

Innocent: Natarajia kuutoa Julai 25, mwaka huu. Ni wimbo ambao nimeutengeneza na kuuandika mimi mwenyewe, maana yake hata jina linajieleza kwamba neema bado ipo kwa Mungu ili watu wasiendelee kutangatanga na mambo ya Dunia kwa sababu neema ipo na anaitoa bure sio kwa pesa. 

Hakuna anayeishi hapa duniani kwa uwezo wake bali ni kwa neema yake Mungu na mimi nimetangaza jina lake sio ufahari wa Dunia hii, nitakapoutoa mashabiki wanaweza kuukuta YouTube hivyo naomba watu waende kusubscribe chaneli yangu ya Innocent v Hope na kusubiri hiyo baraka. 

Swaggaz: Familia yako ina mchango wowote kwenye sanaa yako? 

Innocent: Familia inanipa sapoti kama nilivyosema hapo awali kwamba baba na mama walikuwa ni viongozi wa kwaya na mimi nikawa nawafuata wao. 

Swaggaz: Una mipango gani ya kuendelea kukua kwenye sanaa yako? 

Innocent: Mipango ninayo mingi ila kwa ufupi napanga kufanya muziki bila kuacha naomba Mungu aendelee kuniinua kwenye kipaji changu kwa sababu mkono wake upo juu yangu hivyo ataendelea kunibariki na kuniongoza kikubwa naomba sapoti kwa wapenzi wote wa Gospo. 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles