NEW DELHI, India
TUME ya Uchaguzi nchini hapa, imetangaza kuwa Uchaguzi Mkuu utafanyika mwezi ujao ambao utakuwa ni wa kidemokrasia katika taifa hili na huku ikionekana kwamba, Waziri Mkuu, Narendra Modi, ataibuka mshindi kutokana na mgogoro uliopo baina ya nchi hii na Pakistan.
Akizungumza jana mjini hapa, Msemaji wa tume hiyo, Sunil Arora, alisema uchaguzi utafanyika Aprili 11, mwaka huu na utawahusisha wapigakura milioni 900 na kwamba kati yao, milioni 15 ni vijana wenye umri kati ya miaka 18 na 19.
Katika kipindi cha wiki chache zilizopita, tatizo la uhaba wa ajira na kushuka kwa bei ya bidhaa za kilimo, vilishusha umaarufu wa Waziri Mkuu Modi, lakini wapigakura wanasema Chama Tawala cha Bharatiya Janata Party (BJP), kitawapiku wapinzani wake baada ya mwezi uliopita jeshi la hapa kuingia vitani na wapinzani wa nchi hii, Pakistan na kinaweza kujizolea mamilioni ya kura kutoka maeneo mbalimbali ya nchi.
“Kwa mara ya kwanza nitampigia kura Narendra Modi kwa sababu nimefurahishwa na anachokifanya dhidi ya Pakistan,” alisema Anjali Tivari wakati akimchukua mwanawe kutoka shuleni katika Mji wa Mumbai.
“Nimefurahi sana amewapa jibu sahihi Pakistan,” aliongeza mpigakura huyo.
Akizungumzia uchaguzi huo, Waziri Mkuu Modi alielezea mafanikio ya Serikali na akaelezea kufurahishwa kwake na mwitikio wa watu kujiandikisha kupiga kura.
“Nina matumaini utashuhudiwa uchaguzi wa kihistoria kwa watu wengi kujitokeza. Ninaweza kuuita ni wa kihistoria kwa idadi kubwa ya watu kujitokeza,” aliandika Modi kupitia ukurasa wake wa Twitter.