25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

INAWEZEKANA KUPATA MWONEKANO UUPENDAO KWA KUFANYA MAZOEZI

Dk. Fredirick L Mashili, MD, PhD.

KUMEKUWAPO na taarifa zilizosambaa mitaani kuhusiana na dawa za kukuza sehemu mbalimbali za mwili. Nia ya kukuza au kupunguza sehemu Fulani ya mwili hutokana na msukumo wa kutaka kuwa na mwonekano ambao mtu huupenda.

Si vibaya hata kidogo kama mtu atapendelea kuwa na mwonekano fulani. Tafiti na uzoefu vinaonyesha kwamba, kuwa na muonekano unaoupenda hukufanya ujiamini kitu ambacho hukupa nguvu na ufanisi wa kufanya mambo yako.

Kuna uvumi kwamba kuna wanawake wamekuwa wakitumia dawa ili kukuza sehemu Fulani za miili yao. Inaaminika pia kwamba zipo dawa ambazo hutumika kupunguza tumbo na kumfanya mwanamke kuwa na umbo na shepu ya kuvutia. Kutokana na haya, makala hii itawahusu zaidi wanawake.

Nia si kujadili kama imani hizi ni za kweli au la–bali ni kutaka kuelimishana na kuwataka watu kufahamu kwamba, hata kama dawa hizo hufanya kazi, ziko njia salama na madhubuti zinazomuwezesha mtu kupata umbo alitakalo bila kupata madhara yoyote kiafya.

Ikumbukwe kwamba siku zote vitu virahisi na vinavyopatikana kwa haraka huwa na madhara makubwa.

MAZOEZI YANAWEZA KUKUPATIA UMBO AU SHEPU YA KUVUTIA NA KUKUACHA UKIWA NA AFYA BORA

Huenda umewahi kusikia kwamba mazoezi yanaweza kukusaidia kupata umbo la kuvutia, na ukawa unajiuliza kama hili ni sahihi. Fahamu kwamba dhana hii ni sahihi na hutumiwa na watu wengi kote duniani. Watu maarufu wengi tunaowapenda kutoka katika pande zote duniani–na hata baadhi wa hapa kwetu, hutumia muda mwingi katika sehemu za mazoezi (gyms), nia moja wapo ikiwa ni kutengeneza mwonekano wanao upenda.

Unaweza sasa ukawa ukijiuliza ni vipi mazoezi yanaweza kukufanya uwe na mwonekano unaoupenda. Kwa urahisi kabisa, yale yote tunayoamini huweza kufanywa na dawa, huweza pia kufanywa na mazoezi. Kwa wanawake, mazoezi yanao uwezo wa kuongeza sehemu za nyonga na hata zile za makalio kwa usalama zaidi. Mazoezi yanao uwezo wa kupunguza tumbo/kitambi kwa wanawake na hata kwa wanaume. Cha muhimu ni kuzingatia aina na kiwango cha mazoezi ili ziada ya kupata mwonekano uupendao, upate pia afya bora.

Wakati mazoezi maarufu kwa wanaume ni yale yanayo husisha sehemu ya juu ya mwili (Upper body workouts), kwa wanawake mazoezi maarufu ni yale yanayohusisha sehemu ya chini ya mwili (Lower body workouts). Hii ni kutokana na ukweli kwamba, mara nyingi inapozungumziwa shepu kwa wanawake, kinachozungumzwa zaidi ni sehemu ya chini ya mwili–ikihusisha nyonga, mapaja miguu na hata makalio. Hii haina maana kwamba kifua na sehemu zingine za mwili si muhimu kwa wanawake, ni kutokana tu na kile kilichozoeleka katika jamii.

Hakikisha unapata maelekezo ya jinsi ya kufanya mazoezi ili kufikia malengo yako. Malengo huweza kutofautiana kutokana na kile mtu anachotaka. Lakini kumbuka kwamba ni mchanganyiko wa aina zote tatu za mazoezi ndiyo utakao kusaidia kupata umbo la kuvutia. Ni kawaida kwa wanawake kukwepa kufanya mazoezi ya kusukuma/kunyanyua uzito (resistance exercises), ila kama nia yako ni kuwa na shepu ya kuvutia, huwezi kabisa kukwepa aina hii ya mazoezi.

Fanyavipimovyasehemumbalimbalizamwiliwakokablayakuanzaprogramunajiwekeemalengoyanayotekelezeka. Unaweza pima upana wa nyonga zako, ukubwa wa mkono au hata mzunguko wa mapaja yako. Hivi vyote vitatokana na kile unachokitaka.

Dk. Mashili ni Mtaalamu wa Fisiolojia ya Mazoezi na Homoni. Pia ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Sayansi na Tiba Muhimbili (MUHAS). Kwa maelezo zaidi unaweza wasiliana naye kwa kutumia: namba 0752255949, baruapepe, [email protected]. Unaweza pia kujifunza zaidi kwa kutembelea mojawapo ya tovuti zake: www.jamiihealthtz.com au www.jamiiactive.org

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles