31.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

IGP SIRRO: KIONGOZI AMBAYE ENEO LAKE LITAKUWA NA MAUAJI AKAMATWE

Na TWALAD SALUM-MISUNGWI


MKUU wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Simon Sirro, amewataka viongozi mbalimbali kuanzia ngazi ya Serikali za Mitaa kujitathmini na kuimarisha ulinzi katika maeneo yao na kutoa onyo kuwa yeyote ambaye katika eneo lake kutaendelea kutokea matukio ya mauaji atakamatwa.

Kutokana na kuendelea kuwepo kwa matukio ya mauaji ya kunyongwa wanawake na watoto wilayani Misungwi, IGP Sirro, alionyesha kutokukubaliana na taarifa ya Mkuu wa Wilaya hiyo, Juma Sweda, aliyoiwasilisha ikieleza kuwa hali ya ulinzi na usalama ni shwari.

Sirro aliyasema hayo juzi katika ziara yake ya siku moja wilayani Misungwi, ambapo akizungumza na wananchi kwenye Ukumbi wa MGS katika Kijiji cha Misungwi, alisema hali ya ulinzi na usalama Misungwi si shwari kwa kuwa kuna vifo vya kunyongwa wanawake na watoto.

Kutokana na  hilo, IGP Sirro aliwataka wananchi kuimarisha ulinzi shirikishi kwenye maeneo yao kwa kuwa Jeshi la Polisi lina askari wachache, huku akiwataka viongozi kuimarisha ulinzi kwenye maeneo yao na kujipima kama wanatosha kuwa watendaji kwa kuzuia uhalifu kwenye maeneo yao.

Kutokana na hilo aliagiza kwenye eneo lolote kukitokea mauaji kiongozi wa eneo hilo akamatwe.

“Mimi IGP kuna haja gani kuwepo kwenye nafasi hii iwapo kuna wananchi wanauawa, hivyo hivyo viongozi wengine ngazi ya mitaa, kijiji na wilaya kama wananchi wake wanauawa hafai kuwa kwenye nafasi hiyo,” alisema.

IGP Sirro aliwataka pia wananchi na viongozi kutoa ushirikiano kwenye zoezi linalokuja la kutafuta watu wanaoua akina mama kwa imani za kishirikina na kuwataka wazazi wawakanye watoto wao kujihusisha na uhalifu.

Kwa upande wake, Diwani wa Kata ya Gulumungu, Enosi Mihayo, alisema kwenye kata yake kulitokea mauaji ya kunyongwa wanawake wawili siku moja Juni, mwaka huu na wanafamilia wanaume walikamatwa na polisi na walitakiwa watoe fedha, ambapo walitoa Sh 400,000 kila mmoja na kuachiwa.

“Kuna mtindo hapa Misungwi kuingia rumande bure kutoka ni gharama, tozo hiyo inatambulika kisheria,” alihoji.

Naye Sheikh Mkuu wa Wilaya ya Misungwi, Hussein Hussein, alisema askari polisi wa Wilaya ya Misungwi hawana makazi wanaishi nyumba za kupanga na kusababisha usumbufu wakati wa utoaji huduma za ulinzi, huku Mwakilishi wa chama cha ACT-Wazalendo Misungwi, Flora Marongo, akilalamikia matukio matatu ya vijana kuuawa wakiwa mikononi mwa polisi na kutelekezwa.

Akijibu kero hizo, IGP Sirro, alisema matukio ya vijana kuuawa mikononi wa polisi hakuna mtu aliye juu ya sheria na kutaka taarifa zitolewe wahusika wachukuliwe hatua.

Kuhusu nyumba za polisi, IGP Sirro alisema tayari wamepata Sh bilioni 10 za kujenga nyumba za askari wilayani Misungwi.

MWISHO.

CCM, Chadema watangaza majina ya wagombea Kilimanjaro

Na SAFINA SARWATT

-KILIMANJARO

VYAMA viwili vya siasa mkoani Kilimanjaro, Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), vimetangaza rasmi majina ya wagombea watakaopeperusha bendera katika chaguzi ndogo za marudio ya udiwani kwenye kata tatu.

Kata hizo ambazo zinarudia uchaguzi ni Kata ya Mawenzi iliyopo

Manispaa ya Moshi, Kata ya Makanya wilayani Same na Kata ya Kilemfua

Mkokala iliyopo wilayani Rombo.

Akizungumza na waandishi wa habari, Katibu wa Siasa na Uenezi wa CCM Mkoa wa Kilimanjaro, Mahamoud Karia, aliwataja waliopitishwa kuwa ni Amiri

Mbwambo katika Kata ya Makanya wilayani Same, Kata ya Kelamfua Mokala wilayani Rombo,

Gilbert Tarimo na Kata ya Mawenzi Manispaa ya Moshi, Apaikunda Naburi.

Alisema uteuzi huo wa wagombea hao ulipitia katika mchakato wa kura za maoni kwa mujibu wa taratibu za CCM na hatimaye vikao vya ngazi mbalimbali vilikaa na kuwajadili.

“Vikao hivyo viliwachuja na kutoa mapendekezo yake kwa Halmashauri Kuu ya mkoa ambayo ndiyo yenye mamlaka kikatiba ya kufanya uteuzi wa mwisho wa jina la mgombea atakayepeperusha bendera ya CCM,” alisema Karia.

Mbali na hayo Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa wa Kilimanjaro imewaagiza

madiwani na wabunge wa chama hicho waliopo katika mkoa huo kwenda kusikiliza kero za wananchi katika maeneo yao ya kata na majimbo kwani hicho kitakuwa kigezo cha uteuzi wao mwaka 2020.

Wakati huo huo, Chadema mkoani Kilimanjaro, imetangaza majina ya wagombea wake watakaopeperusha bendera ya chama hicho katika mchakato wa uchaguzi mdogo wa udiwani katika kata mbili huku Kata ya Kelamfua Mokala wakishindwa kutangaza kwa kile walichodai kuwa barua kutoka Tume ya kutoa taarifa ya kufanyika kwa uchaguzi katika kata hiyo kuchelewa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles