30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

IGP MANGU: WAFICHUENI WAHALIFU

Na JUDITH NYANGE-MWANZA


MKUU wa Jeshi  la Polisi nchini (IGP), Ernest Mangu, amewataka wananchi kuendelea kutoa ushirikiano wa kuwafichua wahalifu kwa kutoa taarifa kwa jeshi  hilo zitakazowezesha kukamatwa kwao.

Akizungumza na waandishi wa habari juzi baada ya kumalizika kwa hafla ya kuwatunuku vyeti na zawadi askari polisi 30 wa Mkoa wa Mwanza waliofanya vizuri mwaka jana,  Mangu alisema kazi ya kupambana na uhalifu inahitaji ushirikiano wa kila mtu.

Alisema ili kufanikisha kazi hiyo ni vema wananchi wakaendelea kutoa ushirikiano kwa jeshi hilo kwa kutoa taarifa sahihi kwa siri.

"Kazi ya kupambana na uhalifu inahitaji  usiri, ujasiri mkubwa na ushirikiano wa kila mtu, kama wananchi hawaamini  baadhi ya askari ni vema wakatoa taarifa hizo kwa viongozi wao, " alisema Mangu.

Mangu alisema vita ya kupambana na biashara haramu ya dawa za kulevya inayoendelea nchini inahitaji askari wenye siri na ujasiri, ili kufanikisha kukamata mitandao wa wauzaji, wasafirishaji na watumiaji wa dawa hizo.

"Sitasita kuwachukulia hatua askari watakaokiuka maadili ya Jeshi la Polisi katika vita hii ya kupambana na dawa za kulevya kwa kuwaondoa.

"Najua kwenye msafara wa mamba kenge nao hawakosekani naomba wananchi watupatie taarifa za mienendo ya askari polisi ambao wanakwenda kinyume na maadili ya jeshi la polisi ili tuweze kuwachukulia hatua, "alisema Mangu.

Alisema suala la kuwepo kwa mashamba makubwa ya bangi katika maeneo mbalimbali linatokana na wananchi kukosa ushirikiano na jeshi hilo kwa kuwa hayajifichi na wao wanafahamu kuwepo wake katika maeneo yao.

Kwa upande wake Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza, Ahmed Msangi, amewapongeza wananchi kwa kuwapatia taarifa sahihi ambazo wao huzifanyia kazi  na kuwezesha kukamatwa kwa wahalifu wa makosa mbalimbali.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles