27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

ICC BADO YAWAKALIA KOONI UHURU, RUTO

THE HAGUE, UHOLANZI


MAHAKAMA ya Kimataifa ya Uhalifu (ICC) imechagua majaji wapya kusimamia kesi za Rais Uhuru Kenyatta na naibu wake, William Ruto kuhusu ghasia za baada ya Uchaguzi Mkuu wa 2007.

Ingawa kesi hizo zilikuwa zimesitishwa kwa ukosefu wa ushahidi wa kutosha, Mwendesha Mashtaka Mkuu, Fatou Bensouda, aliambiwa yuko huru kuzifufua endapo atafanikiwa kukusanya ushahidi mpya.

Hiyo ni baada ya kulalamika ushahidi wa awali kuharibiwa na Serikali ya Kenya, ambayo pia iligoma kutoa ushirikiano kuhusu nyaraka mbalimbali, ikiwamo rekodi za simu na benki za Kenyatta.

Mwishoni mwa 2017, ilifichuka wapelelezi wa ICC walikuwa Kenya kuchunguza masuala yanayohusu kesi ya Ruto ambaye alishtakiwa pamoja na mtangazaji wa zamani wa redio, Joshua Sang.

Hilo lilifichuka wakati wa usomaji wa ripoti ya kila mwaka kuhusu shughuli za Ofisi ya Mwendesha Mashtaka Mkuu.

Mahakama hiyo, imefanya mabadiliko ya majaji baada ya majaji sita wapya kuchaguliwa wiki mbili zilizopita huku wengine wakipewa majukumu mapya na baadhi yao kukamilisha muda wao kazini.

Jaji Eboe-Osuji ambaye wiki iliyopita alichaguliwa kuwa Rais wa ICC, sasa atahudumu kwenye kitengo cha rufaa cha mahakama hiyo. Awali alisimamia kesi ya Ruto na Sang.

Kesi hiyo kwa sasa itaendeshwa na majaji Robert Fremr, Reine Alapini-Gansou na Kimberly Prost, ambao pia wataendesha ile ya Rais Kenyatta.

Kwenye taarifa yake kwa vyombo vya habari mwishoni mwa wiki, mahakama hiyo imesema mabadiliko hayo ambayo yameathiri kesi karibu zote zilizo mbele yake, yamechukuliwa kuboresha utoaji huduma.

Taarifa hiyo ilieleza Ofisi ya Rais wa ICC ilizingatia uwezo na weledi wa majaji katika sheria za uhalifu wa kimataifa wakati mabadiliko hayo yalipofanywa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles