23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Huu ndiyo umuhimu wa vitamin A

Na AVELINE KITOMARY-DAR ES SALAAM

UPUNGUFU wa madini ya vitamini A unatishia afya na uhai wa watoto kwa kudhoofisha kinga ya mwili na kuongeza hatari ya kupata magonjwa.

Upungufu huo ni tatizo kubwa la kiafya na jamii hapa nchini na tayari kuna mikakati mbalimbali ya kukabiliana nao imebuniwa.

Lengo kubwa ya mikakati hiyo ni kukabiliana na upungufu wa vitamini A na madhara yake kama vile magonjwa, upofu, upungufu wa kinga mwilini na hata vifo.

Miongoni mwa jitihada zilizofanywa ni pamoja na kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa vitamini A kupitia vyombo vya habari, maonyesho mbalimbali, machapisho, mafunzo kwa watoa huduma za afya, uhifadhi wa vyakula vyenye vitamin A kwa wingi na utoaji wa matone kwa watoto wa miezi 6 hadi 59.

Hivi sasa zoezi la utoaji wa vitamini A linafanyika mara mbili kwa mwaka ambapo utoaji wa matone hayo hufanyika sanjari na utoaji wa dawa ya minyoo kwa watoto wenye umri kati ya miezi 12 hadi 59.

Mkakati huo ukilinganishwa na mikakati mingine unaweza kuwafikia watoto wengi zaidi kwani inakadiriwa kuwa matone ya vita- mini A huokoa maisha ya watoto wapatao 30,000 kila mwaka hapa nchini.

Pia vitamini A hutumika kama tiba kwa baadhi ya magonjwa kama ya macho, surua, magonjwa ya mfumo wa hewa na utapiamlo mkali.

HALI ILIVYO

Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Chakula na Lishe, Dk. Germana Leyna

Mkurugenzi wa Elimu na Mafunzo ya Lishe kutoka Taasisi ya Chakula na Lishe (TFNC), Sikitu Kihinga, anasema tatizo la udumavu bado ni kubwa ambapo asilimia 32 ya watoto wamedumaa huku ukosefu wa vitamini A ukichangia.

“Ina maana kati ya watoto 100 watoto 32 wamedumaa, kwa Tanzania tu watoto ambao ni chini ya miaka mitano wako milioni 9.1 kati ya hao watoto milioni 3.2 wamedumaa hivyo tatizo ni kubwa.

“Mkoa unaoongoza kwa udu- mavu kwa watoto ni Njombe kwa asilimia 46.7 lakini mkoa wenye watoto wengi wenye udumavu ni Kagera ukifuatiwa na Kigoma. Mikoa kama Kagera ina watoto wengi kwa sababu tulichoweza kubaini ni watu kuzaa sana au mwingiliano wa nchi zingine.

“Katika utafiti wetu tume- baini kuwa sababu za udumavu ni mila na desturi, watu wanap- enda kula vyakula vya aina moja mfano unakuta watu wanakula tu ugali, wali au ndizi wanasahau vyakula vyingine kama matunda na mboga,”anasema Kihinga.

Anaeleza kuwa sababu zingine ni watoto kutokuangaliwa na wazazi wao badala yake hulelewa na watoto wenzao hali inayochangia kukosa hata chakula.

“Halafu tabia ya watoto kuacha watoto wawalele watoto wenzao ni tatizo kwani kuna mwingine hamlishi mtoto anakula peke yake na matoto anakula kidogo hapo utakuta mama yupo kwenye biashara au shambani anajua kuwa mtoto wake analishwa lakini kumbe halishiwi vizuri,” anasema.

Ripoti iliyotolewa na Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto (UNICEF) mwaka 2018, inaonyesha kuwa zaidi ya watoto milioni 140 wako hatarini kuugua

kutokana na ukosefu wa vitamini A.Ripoti ya UNICEF inasema katika maeneo yaliyoathirika zaidi utoaji wa matone ya vitamini A umepungua kutoka asilimia 78 hadi 90 mwaka 2009/2015 hadi asilimia 79 mwaka 2015 na asilimia 54 mwaka 2016.

Mkuu wa Mpango wa Lishe wa UNICEF, Victor Aguayo, anasema kupungua kwa maeneo ya watoto waliopatiwa vitamini A kunatishia kuvuruga maendeleo yaliyopatika kwa miongo kadhaa.

Anaonya kuwa mustakabali wa zoezi hilo la gharama ndogo uko mashakani hii ikimaanisha kuwa maisha, uhai na maendeleo ya watoto navyo viko mashakani.

Dozi mbili za matone ya vitamini A za kila mwaka zinaweza kuokoa maisha ya maelfu ya watoto.

Hata hivyo katika mataifa 26 yenye kiwango cha juu cha vifo vya watoto vitamini A inahitajika. Watoto milioni 61 hawakupata vitamini A mwaka 2016 idadi ambayo ni mara tatu zaidi ya mwaka 2015.

Hivyo ripoti imependekeza kuboresha lishe ya watoto na pia kutilia mkazo wa kunyonyesha mtoto kwa miaka miwili ya mwanzo.

UELEWA MDOGO KIKWAZO

Baadhi ya vyakula vyenye vitamin A

Desemba mwaka jana Taasisi ya Chakula na Lishe ilisema pamoja na jitihada nzuri za serikali kwa kushirikiana na wadau bado kuna jamii zenye uelewa mdogo kuhusu umuhimu wa huduma za lishe ya mtoto.

Baadhi ya watoa huduma katika vituo vya kutolea huduma za afya pia wana uelewa mdogo kuhusu manufaa ya huduma wanazotoa hali iliyosababisha kushindwa kutoa elimu sahihi kwa wazazi na walezi wanaowapeleka watoto kupata huduma hizo.

Akizungumza wakati wa mafunzo ya lishe kwa waandishi wa habari mwishoni mwa mwaka jana, Mkurugenzi wa Taasisi ya Chakula na Lishe (TFCN), Dk. Germana Leyna, anasema ushiriki mdogo katika ngazi za jamii ni moja ya chanagamoto ambazo zinatakiwa kufanyiwa kazi ili kumfikia kila mtoto.

Anasema kuwa bado kuna haja ya kuelewa utoaji wa chanjo hiyo unalenga nini kwa watoto na kusisitiza kuwa inatolewa mara mbili kwa mwaka.

“Mawasiliano sahihi ni mojawapo ya zana zinazoweza kubadili mitazamo na tabia za jamii kuhusu huduma ya mwezi wa lishe ya watoto, zoezi hili hu- fanyika mara mbili yaani Juni na Desemba na hutolewa kwa watoto wenye umri wa miaka 6 hadi 59.

“Huduma zinazolengwa ni vitamini A, dawa ya kutibu maambukizi ya monyoo, kupima hali ya lishe, kupima uvimbe unaobonyea katika miguu yote, kutoa rufaa kwa uchunguzi zaidi na kuongeza hamasa kwa jamii kuhusu huduma zinazotolewa,” anasema Dk. Leyna.

Dk. Leyna anasema mwongozo maalumu wa mawasiliano kwa ajili ya watoa huduma za afya vijijini kuhusu utoaji wa matone ya vitamini A na dawa ya minyoo umeandaliwa ili kujenga na kukuza uelewa miongoni mwa wanajamii.

Anafafanua kuwa mwongozo huo pia umekusudiwa kuhakiki- sha ushiriki wa watu na makundi mbalimbali katika jamii kama vile viongozi wa jamii,viongozi wa dini, viongozi wa vyama vya siasa, wazazi, walezi na wanafamilia ili waweze kuchukua hatua mbalimbali kulingana na nafasi zao katika jamii kuhakikisha watoto wote wanaostahili kupata huduma wanapata.

Anasema kuwa huduma hiyo ni muhimu kwa watoto kwani tafiti zinaonesha kuwa vitamini A huweza kuzuia vifo vitokanavyo na sababu mbalimbali kwa asilimia 23, vifo vitokanavyo na surua kwa asilimia 50 na vifo vitokanavyo na maradhi ya kuhara ni asilimia 33.

“Nashauri wazazi na walezi kuhakikisha watoto wao wanapata lishe bora, pia wapate matone ya vitamin A na dawa za minyoo kwani huimarisha kinga za mwili na afya ya mtoto kwa ujumla,” anasema Dk. Leyna.

Pia anasema ni muhimu wa- zazi kuzingatia kuwalisha watoto vyakula mchanganyiko ambao ni mlo kamili ikiwemo vyakula nyenye vitamini A, kuzingatia usafi wa mwili na mazingira na kutayarisha vyakula kwenye mazingira salama.

“Vyakula vyenye vitamini A ni maziwa ya mama, maziwa ya wanyama, mtindi, siagi, jibini, samaki, ini, kiini cha yai na vinavyotokana na mimea ni mboga za majani zenye rangi ya kijani kibichi, matunda yenye rangi ya njano, mafuta ya mawese, mazao ya mizizi kama karoti na viazi vitamu vyenye rangi ya manjano,” anasema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles