24.5 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Hospitali ya Aga Khan yapewa tuzo ya dhahabu

agakhanYASSIN ISSAH NA FLORIAN MASINDE, DAR ES SALAAM

TUME ya Pamoja ya Kimataifa ( JCI ), imeipatia tuzo ya kibali cha dhahabu hospitali ya Aga Khan jijini  Dar es Salaam kwa kufikia kiwango cha  ubora wa huduma kwa wagonjwa ambacho ni sawa na hospitali bora duniani.

Akizungumza katika sherehe hiyo, Mganga Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Profesa Muhammad Kambi,  alisema anaipongeza hospitali hiyo kwa kazi nzuri ya kuinua viwango bora katika utoaji wa huduma inayolenga kuleta athari chanya katika matibabu na kuendeleza sekta ya afya hapa nchini.

“Kwa niaba ya Serikali, napenda kuipongeza hospitali hii ya Aga Khan kwa mafanikio makubwa, nafurahi kwamba kituo cha afya cha Aga Khan kimefanya kazi nzuri kuinua viwango vya ubora katika kuboresha usalama na huduma bora za matibabu hapa nchini,” alisema Kambi

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali ya Aga Khan ya Dar es Salaam, Suleiman Shahabuddin, alisema Mtandao wa Maendeleo wa Aga Khan (AKDN) umedhamiria kuboresha afya Tanzania kwa kufanya kazi na washirika wakuu pamoja na Serikali kuboresha vifaa vyetu vya huduma za afya na kwa vifaa vya Serikali pia.

Alisema mashirika ya Aga Khan na mitandao yake hutoa huduma za afya nchini Tanzania kwa takribani watu 400,000 ndani ya mwaka kupitia hospitali yake, vituo vya afya, miradi ya afya ya jamii na taaluma ya udaktari, lengo likiwa ni kufanya kazi na Serikali na wadau wengine ili kuboresha ubora wa huduma za afya nchini.

Mkurugenzi wa Afya AKDN katika hospitali hiyo, Dk Gijs Walraven, alisema kutoa kibali ni mchakato mgumu na wa muda mrefu, ikiwa na maana kuwa wakati wagonjwa wanaenda hospitali ya Aga Khan ya Dar es Salaam, wanatakiwa wapate huduma bora ya afya kwa kiwango cha juu cha kimataifa.

“Si kila hospitali inafanikiwa kupata kibali cha JCI, vibali hivi hutolewa hospitalini na vituo vya afya kitaaluma kwa viwango vya kimataifa,” alisema Dk. Gijs

Kwa mujibu wa JCI, kila hospitali na shirika la afya lililojiunga nao, huchukua muda wa miaka miwili kujiandaa na kupata kibali, wakati huo shirika zima hufanya kazi kwa pamoja ya kuendeleza na kutekeleza ubora wa hali ya juu na sera ya mgonjwa -salama, mazoea na taratibu sahihi zinazotakiwa kufuatwa ili kufikia viwango vyao.

Aidha, JCI wanatoa vibali hospitalini, kliniki, maabara, huduma za ambulance, mashirika ya usafiri wa dharura, huduma za nyumbani, huduma ya muda mrefu, vituo vya huduma za msingi na vituo vya afya kitaaluma.

Barani Afrika, kuna hospitali tisa za aina hii ikiwamo hospitali ya Aga Khan ya Dar es Salaam na Chuo Kikuu cha Hospitali ya Aga Khan mjini Nairobi, zimepewa vibali baada ya tathmini ya kina ya utendaji wa kitabibu, vifaa na viwango vinavyohusiana na huduma za mgonjwa kuwa ni salama na vyenye ubora wa kiwango cha juu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles