27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

HOJA ZA CAG MWIBA KILA KONA

Na PATRICIA KIMELEMETA-DAR ES SALAAM


HOJA mwiba. Ndivyo unavyoweza kusema hasa baada ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kuvunja ukimya na kutaka kukamatwa kwa Mbunge wa Kigoma Mjini, Zitto Kabwe (ACT-Wazalendo).

Uamuzi huo wa CCM unatokana na taarifa ya uchambuzi wa Zitto kuhusu ripoti ya ukaguzi ya mwaka wa fedha 2016/17 iliyotolewa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Akichambua ripoti hiyo CAG, Zitto alihoji zilipo Sh trilioni 1.5, huku akidai kuwa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) imetangaza mapato yasiyo yake.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Humphrey Polepole, alisema katika uchambuzi na taarifa yake, Zitto amepotosha umma na alivitaka vyombo vya ulinzi na usalama kumchukulia hatua.

“Nimeshangazwa kumsikia Zitto Kabwe akitoa taarifa ya uongo kwa wananchi na kuwadanganya kuwa kiasi cha Sh trilioni 1.5 zimepotea huku akijua kuwa taarifa hiyo si kweli, amepotosha umma.

“Ninavitaka vyombo vya ulinzi na usalama kumwita, kumhoji na kumchukulia hatua kali kutokana na upotoshaji wake,” alisema Polepole.

Wakati Polepole akisema hayo, Zitto alisema yupo tayari kukamatwa na hata kuuawa kwa kusema hivyo kwani mawazo yake hayatakufa.

Licha ya Zitto kutoa kauli hiyo, Polepole, alisema viongozi wa vyama vya siasa wanapotosha ripoti hiyo na inafaa iwekwe utaratibu waanze kuchukuliwa hatua kisheria.

Alisema Zitto ndio anaongoza kupotosha ripoti ya CAG kwa kukurupuka na ripoti asizozielewa na kusema taarifa hiyo walikuwa wameshaipitia.

“Anapotosha kuwa shilingi trilioni 1.5 zimepotea na sasa kuna mtindo mpya ambao unafuata vigezo vya kimataifa vya ukaguzi wa hesabu za umma, unaitaka Serikali inapokagua fedha zake zinapoingia, kuhesabu pia na fedha baada ya Serikali kuwa imetoa huduma.

“Makusanyo ghafi ni makusanyo ya jumla, baada ya makusanyo ghafi inatakiwa ukokotoe ujue makusanyo sahihi ni yapi. Tumekusanya shilingi trilioni 25.3, fedha ambayo huduma imetolewa na inatarajiwa imekwisha kuingizwa kwenye jumla hiyo.

“Ukitaka kujua makusanyo halisi, unachukua shilingi trilioni 25.3 unatoa makusanyo tarajiwa (receivables).

“Unachukua shilingi trilioni 25.3 unatoa shilingi bilioni 687.3 (receivables) kama hatua ya kupata makusanyo halisi.

“Pia unatoa shilingi bilioni 203.92 ambazo ni fedha zilizokusanywa kwa ajili ya Zanzibar, ambayo haisomwi kwenye bajeti ya Serikali ya Muungano

“Ukitoa hesabu hizo, unapata shilingi trilioni 24.4, hizi ndiyo makusanyo halisi ya mwaka 2017/18.

“Zitto anadai pesa zilizotumika kutoka shilingi trilioni 25.3 ni shilingi trilioni 23.79, hii kipindi Mkaguzi anapita zilikuwepo fedha za Serikali ambazo zilikuwa kwenye hatifungani (zilikuwa hazijaiva) ambayo ni shilingi bilioni 697.85.

“Ukichukua shilingi bilioni 697.85 ukijumlisha shilingi trilioni 23.5 unapata trilioni 24.4 na ukichukua shilingi trilioni 25.3 ukatoa trilioni 23.79 unapata shilingi trilioni 1.5 ambayo ndiyo Zitto anadai imeibiwa. Zitto hajui hesabu na anapaswa kumtafuta mwalimu,” alisema Polepole.

Alisema Serikali ilikuwa inadaiwa madeni mbalimbali ya ndani yakiwamo ya wazabuni kiasi cha Sh bilioni 900, lakini ilitumia Sh bilioni 219 kuyalipa baada ya kuhakikiwa na kupitishwa na Bunge.

Polepole alisema kauli ya Zitto ya kudai Serikali imekopa Sh bilioni 500 na kushindwa kulipa, suala hilo analiachia Bunge ili waweze kushughulika nalo.

 Kwa habari zaidi jipatie nakala ya gazeti la MTANZANIA.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles