25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Hoja saba zatawala mjadala wa bajeti

Na RAMADHAN HASSAN-DODOMA

WABUNGE wameendelea kujadili Bajeti Kuu ya Serikali kwa mwaka 2019/20, huku takiribani hoja saba ikiwamo kilimo kuboreshwa zaidi zikijirua.

Hoja nyingine zilizotolewa zaidi na wawakilishi hao ni pamoja na kuendelea kutoa vikwazo vya biashara ili kuwezesha wafanyabiashara wa ndani na nje kufanya shughuli zao, nyongeza ya mishahara na mashine za risiti za kielektroni kutazamwa ili kuondoa kero kwa wafanyabiasra wadogo.

Mbunge wa Mvomero, Seleman Saddiq (CCM), ambaye alisema tatizo lilipo ni ukadirio wa kodi unaofanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na kutokuruhusu wafanyabiashara wanaonunua bidhaa China na Dubai kwenda na fedha taslimu.

“Tulikuwa na Kariakoo ya wafanyabiashara kutoka Malawi, Kariakoo, Burundi, Congo, Uganda na Rwanda, BOT na TRA lazima wajiuelize kuna nini na sababu zipi tulizopoteza biashara Kariakoo,” alisema.


Mbunge wa Chambani, Yusuph Salim Hussein, (CUF)  alisema katika eneo la Kariakoo kuna zaidi ya hoteli 50 ambazo zimefungwa.

Mbunge huyo alisema mwaka jana alichangia hoja bungeni akisema kodi ya milioni 40 kwa kontena inayotozwa bandarini, itaua biashara, kwani wafanyabaishara wanaleta makontena wakidai ya nje ya nchi kisha wanalipa milioni 10 lakini yakifika Uganda, nguo zinarudi Tanzania.

Mbunge wa Gairo,  Ahmed Shabiby (CCM), alisema wafanyabiashara hususan wadogo wanakabiliwa na tatizo kwenye mashine za kutolea risiti za kieletroniki (EFD).

“Mashine za EFD zimekuwa kero, sijajua tatizo ni kampuni zilizopewa tenda au la. Kila siku ni mbovu sasa zimekuwa mtaji kwa watu utaambiwa mashine mbovu nunua nyinge,” alibainisha.

Kwa upande wake, Mbunge wa Ukerewe Joseph Mukundi, (CCM) alisema uchumi unaonyesha kupanda kwa asilimia saba ambazo zilitokana na sekta mbalimbali za uchumi zilizofanya vizuri ikiwemo sekta ya kilimo ambayo imekuwa kwa asilimia 5.3.

“Sekta hiyo inajumuisha mifugo, uvuvi na kilimo lakini bado hakuna uwekezaji wa kutosha huku katika uvuvi bado kuna changamoto ya uwepo wa tozo nyingi zinazosababishwa wavuvi washindwe kuchangia ipasavyo pato la taifa,”alisema Mukundi.

Mbunge wa Viti Maalum, Ruth Molel, (Chadema) alisema watumishi wamesahaulika katika maslahi yao husuasan nyongeza ya mshahara.

“Nazidi kusisitiza watumishi wa umma ndio walipakodi wazuri anapopokea mshahara, analipa kodi bila kukwepa. Nimeangalia bajeti imetengwa kama sh. trilioni saba kwa ajili ya mishahara ikionyesha hakuna nyongeza.

“Kwanini kwenye kodi ya Payee serikali isipunguze kodi hiyo kwa watumishi wanaoitumikia nchi na kuendesha serikali?,”alihoji Molel

Mbunge wa Mtama Nape Nnauye (CCM), alisema uamuzi wa kufuta tozo 54 utasaidi kurahisisha mazingira ya ufanyaji biashara nchini lakini bado kuna tozo nyingine zinapaswa kuangaliwa.

“Pamoja na kufuta tozo ya visima sasa fikirieni kufuta kodi kwenye mitambo ya kuchimba visima vya maji. Mitambo hii itasaidia kuchimba visima pamoja na malango kwa ajili ya umwagiliaji.

“Pia naunga mkono pendekezo la kamati ya bunge kuhusu sekta inayogusa watu wengi ambayo ni kilimo. Ikiguswa inagusa maisha ya watu wengi na ingeweza kupambana dhidi ya umasikini kwa wananchi,” Nnape, alisema.
Mbunge wa Mpwapwa, Geogre Lubeleje (CCM),  alisema fedha za miradi ya maendeleo kwenye mikoa zimekuwa hazifiki kwa wakati, hivyo kusababisha miradi ya maendeleo kukwama.

“Kama fedha hazikwenda kwenye mikoa, Waziri tueleze sababu kama hazikwenda kwa sababu ya majanga, milipuko au magonjwa,”alisema

Kwa upande wake, Mbunge wa Manyoni Mashariki, Daniel Mtuka (CCM) amemshauri mambo manne ambayo yakifanywa na Serikali kwa Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL), zitapatikana fedha nyingi hivyo kuwa tajiri.

Alisema serikali imenunua ndege kubwa sita na inaendelea lakini uuzaji tiketi peke yake haziwezi kuendesha shirika hilo na badala yake kuna shughuli nyingi ambazo zinaweza kufanywa ATCL.

Kwa upande wa Mbunge wa Nzega Mjini, Hussein Bashe (CCM) alimtaka Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philp Mpango, kuangalia  aina ya  sheria zilizopo  kwani nyingi zimekuwa sio rafiki.

“Sasa hatua ya kwanza ninayokuomba Waziri Mpango na najua hii utakumbana na matatizo serikalini, fanya maamuzi yafuatayo,Muite Waziri wa Viwanda na Biashara kaa nae, muombe mfanye mabadiliko makubwa, tuna sheria hapa, tuna sheria ya Camatec, tuna sheria ya TIRDO, tuna sheria ya EPZA, tuna sheria ya TANTRADE, haya ma taasisi yanaji contradict yenyewe, fanyeni harmonization.

“La pili, mtu yeyote anapotaka kusajili biashara, hatua ya kwanza anayofanya ni kwenda sehemu inaitwa Brela. Ushauri wangu, chukueni sheria ya Brela, haya mataasisi yote yawekeni mule ndani, anzisheni kitu kinaitwa business registration licensing & regulatory authority ili mtu anapoingia kusajili biashara, kuchukua leseni anapokutana na kila kitu mule ndani akitoka anaenda kufanya biashara yake.

“La tatu, angalia kitu hiki Mheshimiwa Mpango, GDP contribution, sekta iliyoongoza kukua ni ya sanaa inachangia asilimia 0.3, hii ndio imekua, imengoza kukua katika uchumi wetu. Sekta inayokua ambayo inachangia asilimia kubwa ya GDP, sekta ya kilimo imekua kutoka asilimia 3.7 kwenda asilimia 5,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles