Hatua ya 16 bora  mbungi ya boda boda Cup kutimua vumbi kesho

Na Winfrida Mtoi, Mtanzania Digital 

Michuano ya Tigopesa Mbungi ya Boda Boda Cup hatua ya 16 bora, inatarajia kuanza kutimua vumbi kesho kwenye viwanja vya Bandari, Tandika, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza wakati wa kukabidhiwa vifaa, leo Desemba 7, 2023, Mwenyekiti wa Chama cha Waendesha na Wamiliki wa Boda Boda Mkoa wa Dar es Salaam(CMPD), Michael Masawe, amesema  bingwa wa mashindano  hayo atapata zawadi ya bajaji, kombe na jezi seti moja.

Amesema mshindi wa pili atachukua pikipiki aina 125 TVS ,huku wa tatu akipata pikipiki ya  ya 100 TVS pamoja  seti ya  jezi  kila mmoja

” Leo tumetangaza zawadi na tumegawa jezi kwa timu zetu  16 bora  kuelekea hatua ya 16 bora inayotarajia kuanza kesho, baada ya fainali   kila mmoja atachukua  kile anachostahili,” amesema Masawe.

Ameeleza kuwa  lengo la mashindano ni kuwakutanisha waendesha  bodaboda  na kutoa elimu ya masuala mbalimbali ikiwamo ya usalama barabarani  na matumizi  ya mfumo wa kifedha.

Naye  Ofisa Maendeleo ya Biashara Lipa kwa simu kutoka Tigo,  Nelson Rwehumbiza amesema wametumia nafasi ya michaano hiyo kuwaendeleza kiuchumi  wafanyabiashara wa usafirishaji  ili kuweza kutumia Tigopesa kutunza fedha zao.

“Nia ya Tigopesa ni kuwaendeleza kiuchumi madereva wote waliopo kwenye sekta ya usafirishaji. Tunajua malipo ya fedha tasilimu si salama,pia hatutawapa huduma ya Lipa kwa Simu tu bali tutawapa na huduma za mikopo na bima,” amesema Rwehumbiza.

Kwa upande wa Nahodha wa timu ya CCM Kigamboni, Musellem Omary ‘Dunga’ ametamba kuwa wataondoka na ubingwa huo kwa sababu ya ubora waliokuwa nao, kwani tangu mwanzo mashindano  hawajapoteza mechi.