24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Hapi aiagiza Takukuru kumsaka hakimu anayedaiwa kupokea rushwa

NA FRANCIS GODWIN, IRINGA

MKUU wa Mkoa wa Iringa, Ali Hapi, ameagiza Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kuchunguza na kumchukulia hatua Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Mufindi (jina linahifadhiwa) anayedaiwa kupokea rushwa.

Agizo hilo alilitoa mjini hapa jana baada ya mkazi wa Mtaa wa Mbagala mjini Mafinga, Julius Mwanjigili (42), kulalamika kuwa kesi ya mtuhumiwa wake aliyemjeruhi kwa mapanga imeyeyuka huku akijigamba kumalizana na hakimu huyo.

Hapi alimtaka Kamanda wa Takukuru Wilaya ya Mufindi, Orest Mushi, kuanza uchunguzi mara moja na kuwasaka wote waliohusika kumsaidia mshtakiwa huyo kuachiwa wakati alitiwa hatiani.

Alisema hajapendezwa na hatua ya hakimu huyo na kundi lake kupindisha haki kwa kumsaidia mtuhumiwa huyo kutoka gerezani wakati alikutwa na kesi katika shtaka lililofikishwa mbele yake.

“Siungi mkono wananchi kunyimwa haki zao kutokana na kutokuwa na uwezo wa kulipia ama kununua haki yao kwa kutokuwa na fedha za rushwa za kuhonga hakimu,” alisema Hapi.

Akitoa malalamiko yake mbele ya Hapi katika mkutano wa hadhara wa kukusanya kero, Mwanjigili, alisema kuna ‘danadana’ katika kesi hiyo na ndugu wa mtuhumiwa walidai wamempatia hakimu Sh milioni 1.7 ili kumaliza kesi hiyo na wakaongeza nyingine Sh 300,000 na mtuhumiwa alitolewa gerezani na kutoroshwa.

Naye Mushi alisema agizo la Hapi linaanza kufanyiwa kazi kuanzia leo kwa kumsaka hakimu huyo na wote waliohusika kutoa rushwa ili kupindisha haki ya mkazi huyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles