33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Hamady Kikala: Kombolela ilifanya baba anipe baraka

Na Mwandishi Wetu, Mwanza

MKALI wa Tamthiliya maarufu ya Kombolela, John Elisha maarufu kama Hamady Kikala amesema haikuwa rahisi kwa wazazi wake kukubaliana na kazi yake ya uigizaji lakini baada ya kufanya vizuri kwenye tamthiliya hiyo walimpongeza na kumpa baraka.

John ambaye ni mhitimu wa Stashahada ya Ualimu kutoka Chuo cha Butimba, Mwanza mwaka 2015 ameiambia Mtanzania Digital kuwa aliamua kuchagua sanaa ya uigizaji na kuacha kutuma maombi ya kazi ya ualimu jambo ambalo halikuwafurahisha wazazi wake ambao ni watu wa dini, baba yake, Elisha Ngw’ibombi akiwa mchungaji wa kanisa.

Akivaa uhusika wa Hamady Kikala mtoto wa mwisho wa mzee Kikala katika tamthiliya ya Kombolela ambayo imetamba nchini mwaka jana (2022) ikiruka kwenye chaneli ya Sinema zetu ndani ya Azam TV, John alifanya vizuri na kuwa kivutio kwa mashabiki wa maigizo huku kazi hiyo ambayo ni ya kwanza kufanya na kulipwa vizuri imemfungulia milango zaidi ya kazi za uigizaji.

“Haikuwa rahisi wazazi kukubali kile ninachokifanya kwa sababu rafiki zangu karibu wote wameajiriwa lakini mimi sikuwahi kutuma maombi ya ajira hivyo kila mzazi hupenda kumuona mtoto wake kuwa na maisha bora kwa sababu wanaamini ukiwa mwajiriwa ndipo utatimiza ndoto.

“Baba yangu ni Mchungaji (kanisani) hivyo aliona kijana wake ni kama napotea lakini nilimuomba Mwenyezi Mungu nije nimuaminishe yeye, Mama na jamii kuwa sanaa siyo uhuni bali ni kazi kama zilivyo nyingine,” amesema John na kuongeza:

“Ilichukua muda lakini badaye alinipa baraka zote na kuwa shabiki yangu namba moja juu ya kile ninachokifanya hivyo namshukuru Mungu kwa hilo. Wakati Kombolela inaonyeshwa siku moja Mama alimshawishi akaanza kutazama toka siku hiyo akawa ananitumia ujumbe kunipongeza kwa kazi ni nzuri ilinipa nguvu na akatamka na kunipa baraka kwa mara ya kwanza,”amesema.

Baada ya kufanya vyema kwenye tamthiliya hiyo, John anasema malengo yake ni siku moja kuiwakilisha Tanzania kimataifa kwenye fani hiyo huku akiwataka mashabiki wake kutegemea makubwa na kuendelea kumfuatilia kwani kuna mengi yanakuja mwaka huu hivyo wazidi kuwasapoti wasanii wao wa ndani kwa kufatilia kazi zao.

“Nawashukuru sana watu wote waliochangia kufika hapa nilipo katika sanaa yangu Mungu awabariki. Kwa wanaopenda kunifuatilia zaidi napatikana instagram @officialboneka na youtube channel yangu ni officialboneka,” amesema nyota huyo ambaye ni mwenyeji wa jijini Mwanza.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles