Na Kulwa Mzee-Dar es Salaam
MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imesema kesi inayomkabili Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jamii Forums, Maxence Melo na mwenzake isipoendelea Aprili 3 mwaka huu itafutwa.
Hayo yalisemwa jana na Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba baada ya kukerwa na upande wa Jamhuri ambao ulishindwa kuwasomea washtakiwa maelezo ya awali badala yake ukaomba kuahirisha kesi.
Mwendesha Mashtaka, Inspekta Hamis Said, alidai mbele ya Hakimu Simba kwamba kesi ilitakiwa kuanza usikilizwaji wa awali lakini wakili anayeiendesha anaumwa.
Mwendesha mashtaka aliomba kesi hiyo iahirishwe mpaka tarehe nyingine itakayopangwa.
Hakimu Simba alieleza kukerwa na tabia ya kesi kuahirishwa na kusema wakati mwingine kama kesi hiyo haitaendelea ataifuta.
Aliahirisha kesi hiyo hadi Aprili 3, mwaka huu na dhamana ya washtakiwa inaendelea.
Washtakiwa katika kesi hiyo ni Melo na mwanahisa wa mtandao wa Jamii Media Co Ltd unaoendesha tovuti ya Jamii Forums, Micke William.
Washtakiwa walifikishwa mahakamani na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) kwa tuhuma za kuzuia uchunguzi kwa Jeshi la Polisi.