30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Hakimu amtaka Lissu Kisutu Desemba 19

KULWA MZEE -DAR ES SALAAM

MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Kisutu imesema haitaki siasa, inamtaka aliyekuwa Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu kufika mahakamani Desemba 19.

Uamuzi huo ulifikiwa jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba baada ya kupata taarifa kutoka kwa mdhamini kuhusu afya ya Lissu.

Hakimu Simba alimuuliza mdhamini huyo, Ibrahim Ahmed kwamba mshtakiwa yupo wapi na akajibu kwamba Lissu alikuwa anaumwa, lakini amepona amekataa kuja kwa sababu anahofia usalama wake.

Kabla ya mdhamini kuendelea kuzungumza, Hakimu Simba alimkatisha na kusema mahakama haitaki siasa.

“Sisi hatutaki mambo ya siasa, namtaka mshtakiwa hapa Desemba 19, mwaka huu, siku hiyo Tundu Lissu awepo hapa,” alisema hakimu Simba.

Amri hiyo ilitolewa na hakimu Simba katika kesi ya uchochezi inayomkabili Lissu na wenzake ambao pamoja na mambo mengine wanadaiwa Januari 12 hadi 14 mwaka 2016 katika Jiji la Dar es Salaam, waliandika na kuchapisha taarifa za uchochezi zenye kichwa cha habari ‘Machafuko yaja Zanzibar’.

Jana mshtakiwa Simon Mkina alidai kesi hiyo ina miaka minne sasa na amekuwa akifika miaka yote mahakamani, lakini Lissu hajafika kwa miaka miwili na wanatumia gharama kubwa kwa usafiri na malazi Dar es Salaam kwa kuwa anatokea Mwanza.

Mkina aliiomba mahakama iangalie suala hilo na ione wepesi wa kulishughulikia ili washtakiwa wengine nao wapate nafuu.

Hakimu Simba alisema hata yeye ameandika kwamba kesi ni ya muda mrefu, itajadiliwa Desemba 19.

Awali Oktoba 23, mwaka huu hakimu Simba aliamuru mdhamini wa Lissu tarehe ya jana afike na uthibitisho wa maendeleo ya mshtakiwa.

Kesi hiyo ilifunguliwa Juni 14 mwaka 2016 na baada ya muda mshtakiwa wa nne, Lissu akapata matatizo yaliyomfanya ashindwe kufika mahakamani.

Mbali ya Lissu na Mkina ambaye ni Mhariri wa Gazeti la Mawio, washtakiwa wengine wanaokabiliwa na kesi hiyo ni Jabir Idrisa na Mchapishaji wa Kampuni ya Jamana, Ismail Mehboob.

Lissu na wenzake wanakabiliwa na mashtaka matano likiwamo la kuandika habari za uchochezi kinyume na Sheria ya Magazeti ya Mwaka 2002.

Inadaiwa Januari 12 hadi 14, 2016 katika Jiji la Dar es Salaam, washtakiwa watatu, Jabir, Mkina na Lissu, kwa pamoja waliandika na kuchapisha taarifa za uchochezi zenye kichwa cha habari ‘Machafuko yaja Zanzibar’.

Katika shtaka la pili, wanadaiwa Januari 14, 2016 katika Jiji la Dar es Salaam, walichapisha habari hizo ili kuleta chuki kwa wananchi wa Zanzibar.

Mshtakiwa Mehboob anadaiwa kuwa Januari 13, 2016 katika jengo la Jamana lililopo Manispaa ya Ilala, Dar es Salaam, alichapisha gazeti la Mawio lililokua na taarifa za uchochezi.

Alidai mshtakiwa huyo pia alichapisha gazeti hilo bila ya kuwasilisha hati ya sheria ya kiapo kwa Msajili wa Magazeti.

Mbali na mashtaka hayo, washtakiwa hao kwa pamoja wanadaiwa kuwa Januari 14, 2016, Dar es Salaam, bila ya kuwa na mamlaka yoyote, waliwatisha na kuwatia hofu wananchi wa Zanzibar wasiweze kuingia kwenye marudio ya Uchaguzi Mkuu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles