26.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Fedha za FIFA kulipa madeni ya waamuzi Tanzania

WINFRIDA MTOI, DAR ES SALAAM

SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limesema litaanza kulipa madeni ya waamuzi kuanzia Jumatatu wiki ijayo, wakitumia fedha walizopokea kutoka Shirikisho la Sika la Kimataifa (FIFA).

Kauli hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa TFF, Wilfred Kidao, wakati akitolea ufafanuzi mambo mbalimbali ya shirikisho hilo moja kwa moja kupitia mtandao wao.

Kati ya mambo aliyozungumza kubwa ni kuhusu fedha walizopokea kutoka FIFA, ambazo zimekuwa zikijadiliwa na baadhi ya wadau wa soka kutaka kujua matumizi yake.

Kidau alisema kati ya changamoto zitakazotatuliwa kupitia fedha hizo ni kulipa madeni ya waamuzi wanaodai kwa muda mrefu.

Alisema waamuzi wakataolipwa kupitia fedha hizo ni wale wanaochezesha Ligi Kuu ya Wanawake, Ligi Daraja la Kwanza na la pili, huku wale wa Ligi Kuu Tanzania Bara wakisubiri vyanzo vingine vya mapato.

“Ndani ya wiki moja hii tumekuwa tukiangalia ukubwa wa madeni na jinsi gani tunaweza tukalipa, lakini niwahakikishie kuwa kwa kuanzia tutawalipa waamuzi wa Ligi ya Wanawake, Ligi Daraja la Kwanza na Ligi Daraja la Pili.

“Naamini malipo yataanza kufanyika Jumatatu kwa sababu tumeangukia wikiendi, hivyo kuanzia wiki ijayo kila kitu kitakuwa sawa,” alisema.

Alifafanua kuwa kwa mwaka TFF inapata dola milioni moja sawa na bilioni 2.3 za Kitanzania  ambazo zinatolewa kwa awamu mbili, Januari na Julai.

Kidao alisema kutokana na changamoto ya  janga la Corona, FIFA  imeamua kutoa mapema fedha hizo baada ya kubaini wanachama wake wameathirika na ugonjwa huo.

“Fedha za FIFA huwa zinatoka endapo taasisi husika itakuwa imekidhi vigezo vinavyotakiwa, vigezo hivyo ni pamoja na vile vilivyoanishwa katika uendeshaji wa shughuli kwa kutumia fedha hizo,”alisema.

Alieleza kuwa fedha zinazotoka Januari, mwanachama anatakiwa vigezo vya ukaguzi vya mwaka uliopita, tofauti na zinazotoka Julai.

“Vigezo vingine tofauti na ukaguzi ni  lazima timu ya taifa  iwe imecheza mechi za Kimataifa zisizopungua nne, kuwe na timu za vijana mbili kila moja icheze mechi nne.

“Pia timu za wanawake mbili, nazo zicheze michezo minne ya kimatifa kila moja, kuwepo Ligi za vijana, wanawake ambazo zitachezwa kwa kipindi kisichopungua miezi sita,” alifafanua Kidao.

Alisema pia zifanyike program za waamuzi zisizopungua 10 kwa mwaka, kingine kuhakikisha mwanachama ana mfumo wa usajili uliounganishwa na FIFA.

Kuhusu kurejea kwa Ligi Kuu Tanzania Bara, alisema wanaendelea na vikao kuweka mipango sawa, huku wakisubiri kauli ya serikali.

“Tangu kusimamishwa kwa Ligi, tumekua tukifanya kazi na serikali kwa ukaribu, kuangalia hali inaendaje pia tunatengeneza mipango kuona tutakapo ambiwa turudi tujue tunafanyaje,” alisema.

Aliongeza kwa kusema, walipokea kwa furaha kauli ya Rais wa Tanzania, John Magufuli, kufikiria kurejesha Ligi kwa sababu hata FIFA imewaambia wadau wake kuwa kurudi kwa Ligi kutategemea na kauli ya serikali husika.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles