25.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Fayulu atinga mahakamani kupinga matokeo ya uchaguzi DRC

KINSHASA,    DRC

 MSHINDI  wa  pili wa urais katika uchaguzi mkuu   nchini hapa, Martin Fayulu, juzi aliwasilisha rasmi  pingamizi katika Mahakama ya Katiba kuyakataa matokeo ya uchaguzi akisema   yalighubikwa na udanganyifu.

Fayulu alisema  matokeo ya uchaguzi wa Desemba 30 yaliyotangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi, CENI, yalikuwa yamepangwa na ametoa wito kura zihesabiwa upya.  

 Mahakama ya Katiba ina siku saba za kuisikiliza rufaa hiyo.

  Fayulu anayapinga matokeo ya uchaguzi wa Desemba 30 mwaka jana  yaliyompa ushindi Felix Tshisekedi ambaye  pia ni kutoka upande wa upinzani.

Alisema  Tshisekedi alishinda uchaguzi huo kutokana na mpango wa siri uliofikiwa kati yake na Rais anayeondoka madarakani, Joseph Kabila.

Muungano wa vyama vya upinzani unaoongozwa na Fayulu na unaojulikana kama Lamuka, unadai   kiongozi wao alishinda uchaguzi huo kwa asilimia 61, hiyo ikiwa ni kulingana na waangalizi 40,000 wa uchaguzi kutoka Kanisa Katoliki.

CENI ilisema  Fayulu alipata asilimia 34 ya kura zilizohesabiwa  huku Tshisekedi akishinda kwa kupata asilimia 38.

Fayulu aliwaambia waandishi habari kwamba miongoni mwa mambo anayotaka ni pamoja na kubandikwa  karatasi za matokeo nje ya vituo vya kupigia kura.

Toussaint Ekombe,   wakili wa Fayulu alisema kiongozi huyo anataka yafutwe matokeo ya awali yaliyotangazwa na CENI  na kumpa Tshisekedi ushindi.

Akizungumza juzi  na waandishi habari nje ya mahakama hiyo, Ekombe alisema rufaa hiyo iliwasilishwa  Ijumaa.

Fayulu alisema anaamini   Mwenyekiti wa CENI, Corneille Nangaa alikiuka sheria ya uchaguzi wa Desemba 30 mwaka jana katika kumchagua mrithi wa Rais Kabila.

Hata hivyo, Nangaa alisema kuna njia mbili tu za kuzichukua hivi sasa: moja ni kuyakubali matokeo rasmi ya uchaguzi au kufutwa  uchaguzi huo na kuendelea kumuweka madarakani Rais Kabila hadi uchaguzi mwingine utakapofanyika.

”Wananiita mimi ni askari wa watu na sitowaangusha watu wangu,” alisema Fayulu. Alisema kuwa pingamizi aliloliwasilisha mahakamani linajumuisha ushahidi kutoka kwa mashahidi waliokuwapo kwenye vituo vya kupigia kura.

Katika hatua nyingine,  vikosi vya usalama nchini hapa  viliyazingira makazi ya Fayulu  na kwenye mahakama alikokuwa akitarajiwa kwenda kuwasilisha pingamizi la kuyakataa matokeo ya uchaguzi huo.

 Watu walioshuhudia walisema   wanajeshi na polisi waliyazingira maeneo hayo  kabla Fayulu hajawasilisha pingamizi lake mahakamani.

Wafuasi kadhaa wa Fayulu waliokusanyika nje ya hoteli yake  mjini hapa  pamoja na makazi yake, walikuwa wakiimba nyimbo za kumpinga Rais Kabila pamoja na Rais mteule, Tshisekedi, huku wakihisi kwamba kuzingirwa kwa maeneo hayo ni jaribio la kumtisha Fayulu.

Hayo yalitokea  wakati muungano wa vyama vinavyoiunda serikali    inayoondoka madarakani umepata ushindi mkubwa katika uchaguzi wa wabunge. Matokeo hayo yalitangazwa  juzi alfajiri na CENI.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles