25.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

FANYA UTAFITI AINA YA BIASHARA  ITAKAYOKUFAA

Na  FERDNANDA  MBAMILA-DAR ES SALAAM


HAKUNA  swali  linaloulizwa na wengi  kama ni aina gani ya biashara  ambayo mtu anaweza kufanya ili kufanikiwa na kupata kipato.

Nimekuwa nikisikia maswali  mengi na majibu yake hata mimi nashindwa kupata kutokana na kutokuwa mzoefu na biashara.

Hata hivyo, si kwamba mtu akisomea mambo ya biashara ndio anakuwa na uelewa zaidi kuliko ambaye hajasomea, la hasha! Bali kuna baadhi ya watu huwa na uzoefu au uelewa wa mambo ingawa hawajayasomea darasani.

Hivi  karibuni  nimekuwa nikipata maswali mbalimbali  kuhusu  kama mfanyabiashara anatakiwa kujua kwanza ni aina gani ya biashara ambayo anaweza kuifanya na ikamuingizia faida.

Lakini kuna watu au wafanyabiashara wa karne hii  ambao kwa asilimia kubwa wamekuwa tofauti  zaidi katika uchaguzi na kupanga mipango juu ya biashara gani inafaa kufanya kwa wakati huo.

Kuna baadhi ya watu na haswa wafanyabiashara  walio wengi huwa wanalalamika sana pindi wanapoona kuwa biashara yao inakuwa mbaya zaidi, badala ya kujua na kutafuta tatizo ni nini wanaanza kulaumu na kuanza kuwatuhumu wafanyabiashara wenzake kuwa wanamfanyia hiyana  na kuziba riziki yake.

Imani hizo kwa wafanyabiashara walio wengi zimetawala sana kwani wanashindwa kujua tatizo liko wapi na hatimaye wanashikana  uchawi, na katika biashara nawahakikishia hakuna uchawi wala ndumba kwa wale wanaoamini. Zipo mbinu na njia sahihi za kufanya mambo kwa mikakati bora.

Kikubwa zaidi  ni kujua  mbinu za biashara unayoifanya, inataka  ufanye nini ili ufikie malengo unayoyatarajia kutokana na biashara unayoifanya kwa wakati huo.

Mara nyingi wafanyabiashara wamekuwa wakilalamika bila utafiti kwa kudai kuwa na biashara mbaya lakini ni kutokana na kutokujua tu  na kukosa msingi mzuri wa biashara yako na uwezo wa kuimudu.

Ngoja nikwambie mfanyabiashara mwenzangu unajua siri kubwa ya biashara, ni kujua ni kitu gani wateja wako wanataka katika mazingira hayo na kinachoendana na wakati.

Ingawa kila bidhaa huuzika kwa maana kwamba inategemeana ni aina gani ya mzigo na ni wa gharama gani.

Lakini vilevile kuna baadhi ya bidhaa ambazo unaweza kuweka kwa ajili ya kuuza lakini  nao pia inategemea ni  mzigo wa  aina gani  na unauzia katika mazingira gani.

Hiyo itakusaidia kujua kuwa  unaweza kukaa na mzigo wa biashara yako kwa muda gani toka umeweka kwa akili ya kuuza, kwani kuna bidhaa nyingine  ambazo zilitakiwa  kuisha kuuzwa  ndani ya siku au wiki moja  kwa mfanyabiashara mwingime  huchukua hata mwezi mzima.

Hata hivyo, ni muhimu zaidi kubadilisha aina ya bidhaa kwa ajili ya kuwaletea wateja wako vitu tofauti kwani ukiona biashara unayofanya haikulipi, basi si vyema ukaendelea kuifanya unaweza kufanya  mabadiliko na kuanzisha biashara nyingine.

Nakushauri mfanyabiashara  mwenzangu kuwa  kila biashara  unayoifanya inalipa, kama utazingatia haya basi  katika uchaguzi utakaopanga ni kitu gani au biashara gani unataka uifanye, ni lazima uwe na malengo stahiki hususani kujua ni aina gania ya biashara  ambayo unaweza  kuifanya kwa wakati huo  na iendane na mazingira.

 Hivyo basi,  ni bora mtu kuuliza biashara gani inalipa  badala ya kukurupuka na kuanzisha biashara na  hatimaye inakuja kuanguka na kuanza kulalamika kwa  kupata hasara  ambayo ni matokeo hasi juu ya biashara hiyo.

Ni vyema zaidi  kwa mfanyabiashara wa kiwango chochote kile, kwa maana ya mdogo unaechipukia au mfanyabiashara mkubwa, unakijua unachokifanya katika biashara yako.

Ingawa unaona utaonekana  mjinga kwa kuuliza mambo ya msingi na kufanya vitu ambavyo huvijui na hata vikikushinda inakuwa ni vigumu zaidi kutatua peke yako wakati ungeuliza na kujua ingekusaidia sana katika kuiendeleza biashara yako.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles