Na ODACE RWIMO,
ZAIDI ya familia 1,000 za wafugaji wa kuku wa kienyeji wilayani Igunga zinatarajiwa kunufaika na mafunzo ya teknolojia rahisi ya ufugaji wa kuku, imefahamika.
Mafunzo hayo yatawasaidia kupambana na majanga yanayotokana na mabadiliko ya tabianchi.
Meneja wa Mradi wa Shirika la Exponetial Pass on the Gift (EPOG ), John Toto alikuwa akizungumza kwenye hafla kujadili masuala ya jinsia na upimaji wa VVU katika uwanja wa Sokoine.
Alisema mradi huo unafadhiliwa na Shirika la Mitamba la Kimataifa (Heifer International Tanzania) kwa ushirikiano na Halmashauri ya Wilaya ya Igunga.
Ulianza kutekelezwa wilayani humo katikati ya mwaka 2016 na unatarajiwa kumalizika mwaka 2019, alisema.
Alisema familia au vikundi vitakavyonufaika na mradi huo hadi ifikapo 2019 vitatoka katika vijiji 10.
Alivitaja vijiji hivyo kuwa ni Mbutu, Bukama, Mwabakima, Mwang’halanga, Ibutamisuzi, Igunga, Mwanzugi, Isugilo, Mgongoro na Makomero.
Toto alisema watu 10 walipelekwa Chuo cha Kilimo na Mifugo Tengeru mkoani Arusha ambako walifundishwa utaalamu wa mifugo na ufugaji bora wa kuku wa asili.
“Katika mradi huu halmashauri ya wilaya itatoa wataalamu wa jamii na mifugo kuendesha mafunzo kwa wanavikundi wote kwa wakulima na wafugaji na tayari vikundi 10 kutoka katika vijiji hivyo vimeundwa,” alisema.
Mkuu wa Wilaya ya Igunga, John Mwaipopo, alipongeza jitihada nzuri zinazofanywa na shirika hilo.
Alisema hatua hiyo italeta mwamko chanya wa maisha kwa kushiriki katika masuala ya jamii ikiwamo utunzaji mazingira na kupinga vitendo vya unyanyapaa.
Ofisa Mawasiliano wa Heifer International Tanzania, Mercy Nyanda alisema mradi huo ni mkombozi kwa wananchi wilayani humo.
Alisema mradi utawanufaisha katika uchumi na kuwaepusha na maambukizi mapya ya VVU na vitendo vya unyanyapaa katika familia zao.