DUBAI, UAE
SHIRIKA la Anga la Etihad (EAG) limeandaa kozi maalumu kwa wahandisi na marubani inayofahamika kama ‘Think SciencE 2017’ ili kuhamasisha vijana kupenda masomo ya sayansi na teknolojia.
Tukio hilo lililozinduliwa hapa juzi katika Kituo cha Kimataifa cha Biashara Dubai, limeandaliwa na Taasisi ya Emirates Foundation
Wageni waliotembelea ofisi za shirika hilo walifahamishwa masuala mbalimbali ya uendeshaji ikiwamo jinsi ndege zinavyorushwa.
Aidha walijibiwa maswali mbalimbali waliyouliza kwa marubani na watumishi wa ndege.
Kapteni Salah Al Frajalla wa Shirika la Ndege la Etihad, ambaye pia ni Makamu wa Rais wa Masuala ya Usalama na Shirika la Taifa la Kuendeleza Marubani alisema;
“Hii ni chachu ya maendeleo kwa Falme za Kiarabu (UAE) na dunia kwa ujumla kutokana na kuwahamasisha vijana kujiingiza kwenye taaluma ya urubani.”
“Tunatumaini kuanzishwa kwa Think Science 2017 kutawavutia na kuwatia moyo vijana wengi kuanza kujadili masuala yanayohusu sayansi na teknolojia. Pia kuhimiza vijana wengine kuipenda taaluma hii hata kutamani kujiunga na EAG.”
Katika kuwafanya wageni wavutiwe na kuelewa zaidi kuhusu masuala mbalimbali ya EAG, wageni watapata fursa ya kushindana ili kujishindia safari moja maalumu.
Zawadi zitatolewa kwa vijana watakaoonesha ubunifu kwenye masula ya uhandisi wakati wa mashindano hayo.
Maonesho ya Think Science yalizinduliwa mwaka 2012 yakilenga kundi la vijana wa miaka 15-35 na kuhudhuriwa na maelfu ya wageni kila mwaka.