31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

ENRIQUE AWEKA MAMBO HADHARANI HISPANIA

MADRID, HISPANIA


KOCHA mpya wa timu ya taifa ya Hispania, Luis Enrique, ameahidi kufanya mambo makubwa, ikiwamo kukisuka upya kikosi cha kwanza cha timu hiyo.

Enrique, ambaye alikuwa kocha wa Barcelona, amechukua mikoba ya aliyekuwa kocha wa Hispania, Fernando Hierro, ambaye alifukuzwa baada ya kufanya vibaya katika michuano ya Kombe la Dunia iliyomalizika nchini Urusi.

Hierro alikuwa kocha wa muda baada ya kocha aliyefanikiwa kuivusha timu hiyo kufuzu michuano ya Kombe la Dunia, Julen Lopetegui, kufukuzwa siku chache baada ya kukubali kujiunga na klabu ya Real Madrid.

Katika michuano hiyo nchini Urusi, Hispania ilishinda mchezo mmoja wa makundi dhidi ya Iran na baadaye kuondolewa na Urusi katika hatua ya 16 bora.

“Hayatakuwa mapinduzi, haya ni mageuzi. Kwani unaweza kubadilisha mtindo wa kucheza bila kubadilisha kitu kingine, kama nilivyoonyesha nikiwa Barcelona.

“Soka ni mageuzi endelevu na tuna wazo la kufanya hivyo. Tunaweza kucheza soka nzuri, kuwa na nguvu, kudhibiti mpira na kuwaumiza wapinzani wetu.Kuna vitu tunahitaji kuboresha, pia,” alisema Enrique.

Enrique, ambaye aliwahi kuwa kocha wa Barcelona kati ya mwaka 2014 na 2017 na kushinda mataji mawili, likiwamo Ligi Kuu ya Hispania na Ligi ya Mabingwa Ulaya mwaka 2015, pia aliongeza kuwa, atachagua wachezaji  wenye viwango na aina ya uchezaji wao, lakini si wenye majina makubwa.

“Naona kama nachelewa kutangaza kikosi changu cha kwanza, kitawashangaza wengi, nina uhakika, kikosi cha awamu ya kwanza kitakuwa na wachezaji kama 70.

“Wachezaji wengi miongoni mwao hawatakuwa na uhakika wa kucheza kikosi cha kwanza na sitazungumza na mchezaji yeyote,” alisema.

Miongoni mwa kazi yake ya kwanza kocha huyo itakuwa kumshawishi beki Gerard Pique kuacha mpango wake wa kustaafu soka la kimataifa, baada ya kuahidi kufanya hivyo wakati michuano ya Kombe la Dunia itakapomalizika.

“Pique ni shughuli maalumu, kwani miaka miwili iliyopita alitangaza kujiuzulu. Napenda kuwa na wachezaji wote, akiwamo beki huyo, ameonyesha kuwa na kiwango kizuri, hata hivyo unatakiwa kuheshimu mawazo ya wengine,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles