Na Mwandishi Wetu
Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) kwa kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama, imeteketeza ekari 336 za mashamba ya bangi yaliyokuwa ndani ya hifadhi ya Ikome Wilaya ya Kondoa mkoani Dodoma yakiwa yamechanganywa na mazao mengine halali ili kuficha shughuli hiyo haramu.
Akizungumza wilayani Kondoa wakati wa utekelezaji wa operesheni hiyo, leo Februari 18, 2025 Kamishna Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, Aretas Lyimo ameeleza kuwa, katika operesheni hiyo, kilo 148 za mirungi zilkamatwa.
“Hii ni operesheni kubwa ya kwanza kufanyika mkoani Dodoma, ikionyesha wazi kuwa kilimo cha bangi kimeanza kuenea katika baadhi ya maeneo ya mkoa huu. Tutaendelea kuchukua hatua kali kuhakikisha kuwa uzalishaji, biashara na matumizi ya dawa za kulevya vinadhibitiwa kwa nguvu zote,” amesema Lyimo.
Naye Fatina Ramadhani, Ofisa Mtendaji wa Kata ya Haubi, amekiri kuwa baadhi ya wananchi katika eneo hilo wanajihusisha na kilimo cha bangi na amewaomba waachane na kilimo hicho, kwani matumizi ya bangi husababisha madhara mengi kwa mtumiaji.
Mkazi wa Mafai Kata ya Haubi, Abushekhe Hamis Kalinga amethibitisha kuwa, baadhi ya vijana wanajihusisha na matumizi ya bangi. “Vijana wengi walikuwa wameshaanza kuathirika, japo wengine wanadai wanalima bangi kwa ajili ya pesa lakini ukilinganisha hasara na faida, hasara ni kubwa zaidi kuliko faida. Tusipoangalia kizazi kijacho kitakuwa na watoto wasio na akili timamu,”