30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

ECOBANK YAPANIA 50 KWA 50

Na NORA DAMIAN – DAR ES SALAAM


BENKI ya Eco imejipanga kufanikisha dhana ya ushiriki sawa wa kijinsia kwa kuhakikisha kunakuwepo uwiano wa 50/50 katika ngazi zote.

Suala la usawa wa kijinsia limekuwa likisisitizwa katika kufanikisha ajenda ya Maendeleo Endelevu (SDGs) ifikapo mwaka 2030.

Akizungumza na gazeti hili juzi kuhusu Siku ya Wanawake Duniani, Mkurugenzi Mtendaji wa Ecobank, Mwanahiba Mzee, alisema benki hiyo inatambua umuhimu wa kuwa na uwiano wakijinsia wa wanaume na wanawake kuanzia kwa wafanyakazi wake.

“Hatujafikia malengo ya kidunia lakini kwa kutambua mchango wa wanawake ndio maana tumeifanya hii kuwa ni ajenda kwetu. Tunataka ifikapo mwaka 2030 tuweze kufanikisha 50/50,” alisema Mzee.

Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo, katika nchi 33 barani Afrika ambako Ecobank inafanya biashara wafanyakazi wanawake ni asilimia 44 na mameneja ni asilimia 30.

Alisema bado wanawake wanakabiliwa na changamoto mbalimbali zinazosababishwa na mila na desturi zilizopo ambazo hazimpi nafasi mwanamke kufanya mambo kwa upana wake.

“Wanawake wanakutana na changamoto nyingi sehemu za kazi, nyumbani na kwenye biashara.

“Changamoto ni nyingi lakini tunaweza kuzikabili ndio maana tumejipanga kuhakikisha maisha yanakuwa rahisi kwa wanawake popote walipo,” alisema.

Alisema katika kusherehekea siku hiyo wanatarajia kuwakutanisha pamoja wateja na wafanyakazi wa benki hiyo kwenye kongamano litakalofanyika leo jijini Dar es Salaam.

“Tutasherehekea mafanikio ya wanawake, wataeleza waliyopitia ili kuwapa changamoto wengine,” alisema.

Alisema jamii inatakiwa kupiga vita fikra zote zinazomkwamisha mwanamke na kuhakikisha wanapata fursa na wanakuzwa.

“Maneno ambayo hayatakiwi au hayajengi tuyakemee na kuhakikisha hayaendelei, kama wanawake wamefanya vizuri wapongezwe na wanapopata nafasi waonyeshe mchango wao,” alisema Mzee.

Akizungumzia namna wanavyosaidia jamii, alisema kila mwaka wamekuwa wakitoa sehemu ya faida wanayopata kwa jamii inayowazunguka kama vile kuboresha miundombinu ya maji na elimu.

“Dhamira yetu ni kuunga mkono juhudi za serikali za kuinua kiwango cha elimu hapa nchini na tuna mpango wa kuwafadhili wasichana wanaofanya vizuri ili waweze kufanikisha ndoto zao,” alisema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles