26.9 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

DRAKE, PUSHA T WAPASHA KIPOLO BIFU LAO, NGWEA AKUMBUKWA

NA CHRISTOPHER MSEKENA

IMEKUWA ni wiki ya matukio katika anga la burudani ndani na nje ya Bongo. Mashabiki wameyapa nafasi matukio makubwa ya mastaa kwa kuyajadili  na kufanya yawe gumzo kwa namna moja ama nyingine.

Swaggaz tunakusogezea matukio yote yaliyokuwa gumzo wiki hii kwa kuanzania hapa Bongo na tutamalizia kule Marekani ambako nako kumewaka moto kwa marapa Pusha T Drake kuvuana nguo.

NGWEA AKUMBUKWA

Hili ni gumzo la kumbukizi ya mitano ya kifo cha rapa na mkali wa mitindo huru wa muda wote Albert Mangwea, aliyefariki dunia Mei 28 mwaka 2013 huko, Johanesburg Afrika Kusini kisha mwili wake kurudishwa Bongo na kuzikwa Kihonda,Morogoro Juni 6 mwaka huo.

Moja ya vitu vilivokuwa gumzo wiki hii ni mastaa mbalimbali kutumia nafasi zao kumkumbuka Ngwea kwa uwezo wake kimuziki, ucheshi, utani, kuwa mbele ya wakati, kuishi vizuri na watu pamoja na roho yake safi iliyomuwezesha kuishi na kila mtu katika mazingira yoyote.

Miongoni mwa mastaa ambao hawawezi kumsahau Ngwea, ni Fid Q ambaye ataendelea kumkumbuka rapa huyo kwa kumfutisha mistari mbele ya P Funk Majani wakati wanarekodi wimbo CNN.

Fid Q anasema alilazimika kufuta mistari baada ya kusikiliza mistari ya Ngwea na kugundua kuwa ilikuwa ni mizito kuliko yake.

Ukiacha hilo gumzo la Fid Q, Jumbe nyingi ambazo aliziacha kupitia mtandao wa Twitter, siku moja kabla ya kufa kwake ndiyo zimefanya mashabiki waendelee kumkumbuka zaidi na kuona rapa huyo alikuwa anaaga bila kujua saa kadhaa mbele angefariki dunia.

Miongoni mwa twiti hizo alizoandika Ngwea siku moja kabla ya kifo ni: “ Mambo 5 ya kumfanya mpenzi wako akupende kwa dhati (1) Mpe hela (2) Mpe hela (3) Wewe mpe hela (4) Nakwambia mpe hela (5) We mpe hela tu utaona”.

“Sometimes mambo madogo madogo katika maisha yanaumiza sana kama unabisha kalia sindano”.

Lakini pia siku hiyo mtangazaji Sam Misago alimuuliza Ngwea kama yupo salama maana amekuwa kimya sana naye akajibu : ‘Am perfect bro no worries’ (Nipo sawa kaka hakuna mashaka).

Hizo ndiyo baadhi ya Twitter ambazo wiki hii zimetumiwa na mashabiki wengi kumkumbuka Ngwea ikiwa ni miaka mitano sasa imepita toka lipofariki dunia.

GEORGE TYSON NAYE

Ukiacha Ngwea, mwongozaji na mtayarishaji wa filamu mwenye asili ya Kenya George Otieno Ukumu Tyson, naye amefanyiwa kumbukizi ya kifo chake wiki hii, ikiwa ni miaka minne imepita toka afariki dunia kwa ajali ya gari mjini Morogoro, akiwa katika harakati za kuandaa kipindi cha The Mboni Show kilichokuwa kinaruka EATV.

George aliyezaa na Monalisa mtoto mmoja anayeitwa Sonia, alijizolea heshima kubwa katika tasnia ya filamu kwa kutengeneza filamu kitofauti na waandaaji wengi akiwatumia watangazaji, wasanii wa muziki, wanamichezo na wanasiasa. Filamu kama Girl Friend na Dilema zinazoishi mpaka leo ni miongoni mwa kazi zake.

AY ambaye aliwahi kushiriki katika filamu ya Girl Friend, aliposikia taarifa za msiba huo alikwenda hospitali ya Morogoro na kukuta jeneza aliloliona ni baya, ndipo alipokwenda kununua lingine nzuri kulingana na hadhi ya George (kwa mujibu wa Mboni). Mkali huyo alizikwa kijijini kwao Siaya, Kenya.

PUSHA T & DRAKE

Bifu katika muziki wa rap duniani kote ni kawaida. Mara nyingi hutumika kibiashara pale Mc au rapa anapotaka kuingiza sokoni singo au albamu yake hutumia bifu bandia kuongeza usikivu na msukumo wa mashabiki kuitafuta bidhaa hiyo.

Wiki hii nchini Marekani rapa Pusha T na Drake wamepasha kipolo bifu lao lililoanza mwaka 2012, kwa wawili hao kukosoana katika muziki wao japo ilikuwa kimya kimya lakini hivi sasa wameamua kuliweka wazi kupitia mitandao ya kijamii.

Kupitia wimbo Infrared Pusha T, alim ‘diss’ Drake kuwa hawezi muziki kwani anaunga unga mistari kama ushindi wa Trump huku akiwatumia ‘Gostwriters’ (Watunzi wa nyimbo) kumwandikia nyimbo kitu ambacho kilimuudhi Drake.

Drake naye alijibu kwa kupitia ‘Duppy Freestyle’, aliyoitoa akiwachana Pusha T na Kanye West, kitu ambacho aliwahi kukifanya siku za nyuma alipokuwa kwenye bifu na Meek Mill.

PUSHA T AJIBU, DRAKE ATULIA

Jumatano wiki hii Pusha T alimjibu Drake kwa kuachia wimbo The Story of Adidon ambao alisampo ngoma The Story of OJ wa Jay Z huku kava ikitumika picha ya Drake akiwa amepaka rangi nyeusi.

Pusha T alidondosha dongo kwa Drake kuwa ametelekeza mtoto wake wa kiume aliyezaa na Sophie, ambaye ni mcheza filamu za ngono.

Mpaka sasa Drake hajajibu chochote kitu ambacho kimezua gumzo kwamba Pusha T, amegusa kwenye ukweli na sasa anatazamiwa Champagne Papi huwenda atajibu tuhuma hizo katika albamu Scorpion, inayotarajia kutoka mwezi huu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles