23.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

DOGO MFAUME AMEKWENDA NA MUZIKI WAKE

NA CHRISTOPHER MSEKENA

KATIKATI ya wiki hii muziki wa Bongo Fleva ulipata pigo la kuondokewa na msanii wake aliyejipatia umaarufu kwa kufanya aina ya kipekee ya muziki unaoitwa mchiriku au mnanda. Huyu ni Suleiman Mfaume, maarufu kama Dogo Mfaume, staa wa singo ya Kazi Yangu ya Dukani.

Dogo Mfaume ni sampuli za wasanii adimu mno kutokea kwenye tasnia ya muziki nchini toka ulipoanza kupata mashiko kwenye jamii. Mchiriku au mnanda ni aina ya muziki ambao haupatikani popote pale zaidi ya Tanzania.

Aina hiyo ya muziki imebeba maisha halisi ya asilimia kubwa ya Watanzania wanayoyaishi, hata mambo ambayo yanaimbwa ndani yake yanawagusa moja kwa moja Watanzania.

Mfano ni wimbo huu wa Kazi Yangu ya Dukani, utaona ni jinsi gani Watanzania walimpokea na kumpa nafasi kwa kuwa alichokiimba kwenye ile singo ni tabia ambayo ipo kwenye jamii na watu wanaendelea kukopa na muda mwingine wateja wamekuwa wakisababisha maduka kufilisika.

Nisingependa sana kuzungumzia ustaa ulivyomlevya Dogo Mfaume kiasi kwamba akajikuta anaingia kwenye utumiaji wa dawa za kulevya, ila napenda wasanii na vijana wajifunze kupitia kosa alilolifanya mfalme huyu wa mchiriku ili nao wasimezwe na janga hilo.

Ila napenda kumzungumzia Dogo Mfaume kama msanii aliyethubutu kuutoa mziki wa mchiriku kule mtaani mpaka ukafika kiwango cha kuchezwa kwenye vyombo vya habari kama redio na runinga, huku ukiwa umebeba Utanzania.

Heshima sana kwa Dickson Ponela na mtayarishaji Man Water kwa kuweza kumpokea Dogo Mfaume na kumtengenezea jukwaa la Watanzania kumwelewa. Ilikuwa hivyo na hakika muziki wa mchiriku ulifanya Watanzania nao wasimame na kutamba kuwa na aina ya muziki ambao unapatikana nyumbani tu.

Lakini sasa muziki huo hauna tena mwakilishi, utakosa mwelekeo na unaweza kufa kabisa kwa sababu Dogo Mfaume pekee alibaki hai na ndiye aliyekuwa anaijua ramani sahihi ya mwelekeo wa muziki huo wa Kitanzania.

Nikukumbushe kuwa, hata wanamuziki kama Juma Mpogo na Omary Omary nao hatupo nao leo, hivyo hakuna staa  mwingine anayeweza kuendelea kufanya aina hiyo ya muziki wenye ladha ya kipekee.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles