27.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

DNA YAMZULIA JAMBO MCHUNGAJI MSIGWA BUNGENI

Fredy Azzah, Dodoma

Mbunge wa Iringa Mjini, Mchungaji Peter Msigwa leo ameharibu hali ya hewa bungeni wakati akichangia Hotuba ya Bajeti ya Ofisi ya Rais, Utawala Bora, baada ya kusema viongozi walio kwenye ofisi za umma hawana sifa ambapo kabla hajamalizia baadhi ya wabunge walianza kuzomea wakisema; ‘DNA, DNA’.

Hali hiyo iliendelea na kumfanya Mchungaji Msigwa kukatishwa mara kadhaa na wabunge waliokuwa wakiomba mwongozo na wengine kutoa taarifa, jambo lililofanya Mwenyekiti wa Bunge, Najma Giga kutumia muda mwingi kuwatuliza wabunge waliokuwa wakizomea ama kuangua vicheko.

Hali ya hewa ilianza kuchafuka baada ya Mchungaji Msigwa kusema; “unamchukua mtu kama Kitila (Kitila Mkumbo, Katibu Mkuu Wizara ya Maji) unampeleka kwenye Wizara ya Maji, anakaa ofisini badala ya kuzungumza mambo ya kumtua mama ndoo ambalo ni wazo zuri, yeye anakazana anataka amjibu askofu kwa sababu ya mawazo aliyotoa kwamba hakuna demokrsia,”.

Mchungaji Msigwa alikatishwa na Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Injinia Stella Manyanya, aliyeomba mwongozo akisema mzungumzaji anaingiza jambo ambalo halipo kwenye mjadala.

“Mheshimiwa tunza heshima yako usiharibu hii ajenda, jikite kwenye ajenda iliyo mezani,” alisema Injinia Manyanya.

Baada ya Mwenyekiti kumruhusu Msigwa kuendelea kuzungumza, alianza kwa kusema “haya ndiyo mambo ninayozungumza, dada yangu namheshimu sana na ni mhandisi lakini anashindwa kuunganisha utawala bora ninaozungumzia na mifano ninayotoa, hizi ndiyo appointment (uteuzi) ninazozungumzia, yaani haelewi kabisa”.

Wakati akiendelea kuchangia, ziliendelea kusikika sauti za baadhi ya wabunge wakisema DNA, DNA.

Msigwa aliendelea kusema; “mtu kama Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Alexander Mnyeti, anatumia vibaya ofisi ya umma kwa kugawa kadi za CCM na kusema hatashirikiana na wapinzani huo si utawala bora”.

Baada ya kauli hiyo, Mbunge wa jimbo la Kasulu Vijijini, Vuma Augustino,  aliomba kumpa taarifa Msigwa ambapo alisema Mkuu wa Mkoa ni mjumbe wa kamati ya CCM ya mkoa hivyo ana haki ya kutimiza wajibu wake.

Msigwa alimjibu kwa kusema anarudia kuwa hayo ndiyo alikuwa akiyazungumzia, na kumuita mbunge huyo kuwa kijana mdogo msomi lakini anashindwa kutofautisha kazi ya Mkuu wa Mkoa na shughuli za CCM na kuongeza kuwa hiyo  ni huzuni hawezi kuelewa.

“Unamchukua mtu kama Makonda (Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda), kila siku anaharibu, alianza madawa ya kulevya….,” sauti za DNA, DNA zilianza tena na wakati huu zikiwa nyingi zaidi na kumfanya ashindwe kuzungumza.

Mwenyekiti wa kikao hicho, alitumia takribani sekunde 10 kutuliza wabunge.

Msigwa aliendelea kuzungumza akisema kama suala ni DNA yuko tayari na anaweza kushughulika vizuri, huku kelele nyingi zikisikika kutoka upande wa CCM.

Baada ya hapo, Mbunge wa Siha Dk. Godwin Mollel, aliomba kutoa taarifa ambapo kabla hajasimama kuanza kuzungumza, Msigwa alisikika akimuuliza “kwani Mollel na wewe unataka kupimwa mbegu,” jambo lililozua kelele zaidi.

Akitoa taarifa yake, Dk. Mollel alisema wabunge hao wa Chadema wanachangishwa Sh milioni 75 kwa mwezi lakini wameshindwa kuajiri watu wanne wa kuwaandalia hotuba zao.

Wakati akiendelea baadhi ya sauti zilisikika zikisema “Dk. Shika, Dk. Shika” hali iliyosababisha wabunge wengi zaidi kuangua vicheko.

Baada ya wabunge kutulia, Dk. Mollel alisema; “mimi siendi kwenye DNA kwa sababu ni mambo binafsi,” kauli hiyo ilifanya aendelee kuzomewa jambo lililomkatisha kwa muda na baadaye kuendelea kwa kusema “umesikia mazuzu na misukule wananizomea.”

Kauli hizo zilifanya wabunge waangue kicheko huku wengine wakisema; “njaa, njaa,”.

Msigwa alipopewa nafasi ya kuendelea kuzungumza alianza kwa kusema anaomba kumsaidia Dk. Mollel huku akimuita bidhaa anayenunuliwa kama karanga barabarani huyu, mwanaume mzima ananunuliwa kama karanga.

“Hotuba ya Serikali haijaandaliwa na waziri imeandaliwa na timu kubwa, leo mnataka sisi tuandae kwa dakika moja kwasababu mnaona tunafanya mchezo hapa, nakupuuza wewe sijui Dokta wa wapi wewe,” alisema Msigwa.

Baada ya kumaliza kumjibu Mollel, aliendelea na mjadala wake akizungumzia ushauri waliotoa kwa serikali juu ya sekta ya madini.

Hata hivyo, alikatishwa tena na Jackline Ngonyani, aliyeomba kutoa taarifa akasema “nilitaka kumwambia Msigwa utawala bora anaozungumzia ni suala la msingi, lakini unapoanza kunyoosha kidole kwa mwenzako vidole, vingine vinakurudia wewe, angeanza mwenyewe kwenye suala la DNA, Dar es Salaam ameshaenda  na yule inasemekana ni mke wa mtu.”

Msigwa alipopewa nafasi ya kumjibu alisema “nataka nimwambie Mbunge, mama niko vizuri sana, kama unataka suala la DNA niko vizuri labda kama unataka vitu vingine nako niko vizuri.

“Anayetaka kuja aje tu, kama mnadhani hiyo ni kiki mnapoteza muda, sasa na Mawaziri wote tutawapima DNA humu ndani si mnataka tupimane, hamna shida.

“Ninachozungumza ndiyo haya, tunaacha kuzungumza mambo ya msingi ya nchi, tunazungumza mambo ya msingi watu wanakufa mnahangaika na DNA yangu,” alisema Msigwa.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles