27.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

Dk. Shein: Tutapambana na rushwa kwa nguvu

MWANDISHI WETU-ZANZIBAR

RAIS wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein  amesema suala la kupambana na rushwa lina umuhimu mkubwa katika maendeleo ya nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki hasa ikizingatiwa   vitendo hivyo vinazorotesha uchumi na maendeleo.

Aliyasema hayo jana alipozindua Mkutano wa Nne wa Bunge la Afrika Mashariki (EALA) unaofanyika kwa mara ya kwanza kwenye Ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani mjini hapa.

Dk. Shein alisema kuwapo Muswada wa Rushwa katika mkutano huo kwa mwaka huu ni jambo muhimu kwa vile  utasaidia kupambana na vitendo vya rushwa ambavyo vimekuwa vikiathiri uchumi na maendeleo ya nchi na wananchi wake.

Alisema   muswada huo unakwenda sambamba na juhudi mbalimbali zinazochukuliwa na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki katika kuendeleza mapambano dhidi ya rushwa na uhujumu wa uchumi.

“Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika jitihada zake za kukomesha vitendo vya rushwa imeunda Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi Zanzibar (ZAECA) kwa lengo la kushughulikia suala zima la kupambana na rushwa.

“Juhudi hizo zinaendelea kwa ushirikiano wa pamoja na wananchi hatua ambayo imesababisha  mamlaka hiyo kuweza kupiga hatua kubwa,” alisema Dk. Shein.

Alisema hata Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais Dk. John Magufuli,  imeongeza juhudi katika kuimarisha mapambano dhidi ya rushwa kwa kuweka mikakati mbalimbali.

 “Juhudi hizo zitasaidia  pamoja na zile sheria zitakazotungwa na Bunge hili ambazo zote kwa pamoja zinaweza kufikia lengo lililokusudiwa,” alisisitiza Dk. Shein.

Dk. Shein aliwaasa wajumbe wa Bunge la EALA kuzingatia umhimu wa maadili na tabia njema katika kutekeleza majukumu yao hasa wakati huu ambao teknolojia na mifumo ya maisha imebadilika.

Alisema inatia moyo kuona  ukanda wa Afrika Mashariki ni miongoni mwa kanda zinazoongoza katika ukuaji mzuri wa uchumi duniani.

Dk. Shein alisema  katika mwaka wa 2017 uchumi ulikua kwa asilimia 4.6 ikilinganishwa na mwaka 2016 ambako  ulikua kwa asilimia 4.4.

Alimhakikishia Spika wa Bunge hilo, Martin Ngonga kuwa SMZ itaendelea kuwa mstari wa mbele katika kuendeleza na kuitangaza lugha ya Kiswahili.

Alisema  kupitia Baraza la Kiswahili la Zanzibar (BAKIZA) imekuwa ikiandaa makongamano mbalimbali ya Ksiwahili ambayo yanajumuisha wataalamu kutoka sehemu mbalimbali duniani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles