-ZANZIBAR
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, amekutana na uongozi wa Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na kukamilisha vikao vya kupitisha Mipango ya Utekelezaji wa Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya mwaka 2015-2020 vilivyoanza wiki iliyopita.
Katika kikao hicho kilichofanyika mjini Unguja jana, Dk. Shein aliwapongeza viongozi na watendaji wa ofisi hiyo kwa kufanyakazi kwa ushirikiano ambao alisema umekuwa msingi wa mafanikio ya utekelezaji wa majukumu ya ofisi.
Alisema katika miaka mitano ya kwanza ya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar awamu ya Saba, ofisi hiyo ilitekeleza vema majukumu yake ya kutekeeleza Ilani.
Hata hivyo alitoa wito kwa viongozi na watumishi kuongeza kasi katika kipindi hiki cha pili cha Utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi kwa mwaka 2015-2020.
Aliitaka ofisi hiyo kuhakikisha kila idara ya ofisi hiyo inakuwa na watumishi wa kutekeleza majukumu ya idara kisiwani Pemba kuwe na uwiano sahihi wa utekelezaji wa Ilani Unguja na Pemba.
Dk. Shein pia aliitaka Kurugenzi ya Mawasilianao Ikulu kubuni njia nyingi na rahisi zaidi za kuwasiliana na wananchi kuendelea kuwaweka karibu serikali.
“Pamoja na kazi nzuri inayofanywa kuwapatiwa wananchi taarifa mbalimbali kuhusu shughuli za serikali kupitia njia mbalimbali za mawasiliano ipo haja ya kubuni njia nyingine rahisi ambazo zitapanua wigo wa mawasiliano kati ya Serikali na wananchi.
“Taarifa muhimu za Serikali hazina budi kuwafikia wananchi kwa wakati na kwa uhakika ikiwezekana kutumia mfumo wa utawala kupitia kwa masheha na baadhi ya machapisho yanaweza kuwasilishwa kwao na kugawanywa kwa wananchi,” alisema Dk. Shein.