30.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Dk. Rashid: Kisukari bado tishio

Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Seif Rashid
Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Seif Rashid

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

SERIKALI inakusudia kuongeza bajeti ya fedha za kununua dawa za kutibu kisukari kwa kuwa ugonjwa huo umeshakuwa tishio hapa nchini.

Akizungumza Dar es Salaam jana katika Mkutano wa Pili wa Pan African Diabetic Foot Study Group, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk. Seif Rashid, alisema fedha hizo zitanunua dawa zitakazotolewa bure kwa wagonjwa wa kisukari.

Alisema licha ya dawa za ugonjwa huo kuwa za gharama kubwa, upatikanaji wake nao mgumu.

Alisema Serikali itajitahidi kuweka kliniki za kisukari katika hospitali za wilaya ili wagonjwa wasihangaike kwenda umbali mrefu kupata huduma katika hospitali za mikoa.

“Serikali imeutambua ugonjwa wa kisukari kama moja ya magonjwa yasiyoambukiza ambayo wagonjwa wake wanapaswa kupewa dawa bure, nia ya dhati ipo ila fedha bado ndiyo tatizo katika kutekeleza nia hiyo,” alisema Dk. Rashid.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Pan African Diabetic Foot Study Group, Dk. Zulfiqarali Abbas, alisema Tanzania ni miongoni mwa nchi zenye mzigo mkubwa wa wagonjwa wa kisukari.

“Tanzania ina mzigo mkubwa wa magonjwa yasiyoambukiza, sio tu kisukari bali na matatizo yanayoambatana na ugonjwa huu kama vile vidonda vya kisukari miguuni ambalo ongezeko lake haliwezi kufumbiwa macho,” alisema Dk. Abbas.

Kuhusu mkutano huo, alisema wajumbe wake wanatoka nchi tisa za nje ya Bara la Afrika, wajumbe 29 kutoka nchi za Afrika na wajumbe kutoka mikoa 26 ya Tanzania.

Alisema lengo la mkutano huo wa siku tatu ni kutoa taarifa zilizopo kwa wakati huo kuhusiana na kinga na matibabu juu ya vidonda vya kisukari miguuni katika Afrika.

Alisema wasemaji tofauti ambao wapo katika nyanja hiyo ya vidonda vya kisukari miguuni, watawasilisha hotuba adilifu na mbali na hotuba hizo pia kutakuwa na maonyesho ya vitendo jinsi ya kuhudumia vidonda vya kisukari miguuni.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles