23.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Dk. Mwinuka: Sitawavumilia wazembe Tanesco

MWANDISHI WETU-DODOMA

MKURUGENZI Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Dk. Tito Mwinuka,  amesema hatawavumilia watumishi wazembe ndani ya shirika hilo na kwa sasa siku zao zinahesabika.

Hayo ameyasema leo Jumanne Januari 14, jijini Dodoma wakati akifungua mafunzo ya siku sita kwa watumishi wapya 958 walioajiriwa hivi karibuni.

Watumishi hao wanaendelea na semina elekezi wakiwa na wakufunzi kutoka Chuo cha Utumishi wa Umma na wako katika vituo vitatu ambavyo ni Dodoma, Morogoro na Mtwara.

Dk. Mwinuka alisema Tanesco ni shirika linalotegemewa katika ukuzaji wa uchumi wa taifa, hususani katika kipindi hiki ambapo nchi inaelekea kwenye uchumi wa viwanda, hivyo haiwezekani wengine wakawa wanakimbia halafu mwingine anatembea au amekaa.

Alisema watumishi hao wapya ni lazima watambue kuwa Serikali inawategemea zaidi kwa kuwa wameingia ili kuongeza kasi ya kufikia malengo ya kuzalisha megawati 10,000 ifikapo mwaka 2025.

“Serikali ina matumaini makubwa kutoka kwenu, mmeingia katika eneo linalotazamwa zaidi na wengi na kutegemewa, hivyo lazima mtambue Serikali inategemea nini kutoka kwenu ili msiliangushe shirika,” alisema Dk. Mwinuka.

Kwa upande wake, Mkuu wa Chuo cha Utumishi wa Umma, Dk. Emanuel Shindika, alisema mafunzo kwa watumishi hao wapya yanalenga kuboresha mifumo ya utendaji wao katika utumishi.

Dk. Shindika alisema utumishi wa umma ni jambo jema kwa mtu anayeweza kuwatumikia watu, lakini itakuwa aibu kwa anayeshindwa kufuata maadili na vigezo vya kiutumishi wakati wote.

Aliwataka watumishi hao kuzingatia watakayofundishwa ili wanapofika kazini wasiwe na shida kwani semina elekezi huwa ni zaidi ya mafunzo ya vyuoni.

Kwa niaba ya washiriki wenzake, Astelia Sukulu alisema mafunzo hayo yatawasaidia kujua miiko na wajibu wao katika chombo cha umma, lakini akisisitiza watakuwa wenye kutunza siri za shirika.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles