30.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Dk. Masha: Nilikosa ajira sababu ya Nyerere

Dk. Fortunatus Masha
Dk. Fortunatus Masha

NA ABUBAKARI AKIDA, MWANZA

BAADA ya kimya kirefu, hatimaye aliyewahi kuwa Katibu Mwenezi wa kwanza wa TANU na baadaye kufukuzwa katika chama hicho mwaka 1968, Dk. Fortunatus Masha, ameibuka na kusema matatizo yaliyokuwapo kati yake na Mwalimu Julius Nyerere yalichangia asipate ajira ndani na nje ya Afrika Mashariki.

Dk. Masha ambaye kwa sasa ni mwanachama wa Chama cha UDP, alisema hayo katika mahojiano maalumu na MTANZANIA yaliyofanyika jijini hapa ambapo pamoja na mambo mengine aligusia uhusiano wake na Mwalimu Nyerere ulivyokuwa kabla na baada ya kufukuzwa TANU.

Agosti 1968, Mkutano wa Halmashauri Kuu ya TANU uliofanyika mjini Tanga uliridhia kwa kauli moja kufukuzwa uanachama kwa Dk. Masha na wanachama wengine maarufu wa chama hicho zaidi ya wanane kwa kile kilichodaiwa kulipinga Azimio la Arusha.

Pamoja na Dk. Masha, wengine waliofukuzwa TANU wakati huo ni Oscar Kambona ambaye baadaye alikimbilia uhamishoni nchini Uingereza, Joseph Kaselabantu, Eli Anangisye, Wilfram Mwakitwange na wengine waliotajwa kwa majina mojamoja ambao ni Choga, Kaneno, Bakampenja na Kiguga.

Wakati akifukuzwa TANU, Dk. Masha alikuwa pia ni mwajiriwa wa Wizara ya Habari.

Katika mazungumzo hayo huku akionekana kuguswa sana, Dk. Masha alisema baada ya kufukuzwa TANU, Serikali iliagiza asipewe ajira ndani na nje ya Afrika Mashariki na kusisitiza hiyo ni sababu iliyomfanya kuondoka nchini.

Alisema baada ya kukosa ajira kila anapokwenda kuomba kazi ikiwamo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, alilazimika kurejea kijijini kwake Kamanga na kuanza kazi ya kufuga ng’ombe na kilimo.

“Baada ya kufukuzwa chama na kupoteza ubunge wangu wa Geita Mashariki, nilianza kutafuta kazi, niliomba sehemu nyingine, niliomba kazi kama Afisa Mahusiano katika Shirikisho la Viwanda lililojulikana kama National Development Cooperation (NDC), lakini nilikuta maagizo ya Serikali kwamba nisipewe ajira hapa nchini.

“Niliambiwa kila nilikoomba kazi kuwa maagizo toka serikalini nisipewe kazi. Nikaamua kutoka nje ya nchi na nikaenda Jumuiya ya Afrika Mashariki kuomba ajira, nako pia nikakuta maagizo yale yale kwamba Serikali imeleta maagizo ya kwamba wasinipe ajira.

Dk. Masha alisema kuwa wakati akiwa Nairobi akielekea masomoni nchini Marekani, alimwandikia Mwalimu Nyerere barua akimwambia anakoelekea, alikopata pesa za kumsemesha.

“Sikukimbia na ndiyo maana nilirudi kuja kuichukua familia yangu,” alisisitiza.

- Advertisement -

Related Articles

3 COMMENTS

  1. Uliyoyasema ndugu Philipo ni kweli tupu,wengi wanaofukuzwa kazi kutoka katika vyama vya siasa au serikalini tunashuhudia mafanikio makubwa wanayoyapata, hasa ikiwa kufukuzwa kwao kunatokana na matendo na mawazo yao ni kwa ajili ya kuliendeleza Taifa na sio kujinufaisha binafsi na familia zao. Yuko wapi Mh.Aboud Jumbe, Ramadhan Haji,Mansour na Othman Masoud?

  2. Nyerere did the right thing nchi yetu ingekuwa kwenye civil war, since then alicho kuwa anataka ni stability na siyo kujinufaisha kama hao wachache wasivyo taka.

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles