31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Dk. Bashiru ataka mchujo mkali wagombea udiwani, ubunge CCM

Amina Omar -Kilindi 


CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimewataka viongozi wake kusimamia uchujaji wa wagombea wa nafasi za udiwani na ubunge kwenye maeneo yao ili kupata wagombea wenye sifa.

Hayo yalielezwa na Katibu Mkuu wa CCM, Dk. Bashiri Ally, katika kikao chake na viongozi na wanachama wa chama hicho kilichofanyika jana Wilaya ya Kilindi mkoani Tanga.

Dk. Bashiru aliwataka viongozi hao kutumia muda wao kufanya kazi za chama badala ya majungu na fitina na waepuke kuwa na majina ya wagombea kwenye mifuko yao.

Aliwakumbusha Watanzania asili ya CCM ni
chama cha wakulima na wafanyakazi ambao alisema bado hawajapewa heshima inayowastahili.

Akizungumzia kinyang’anyiro cha uchaguzi mwaka 2020, Dk. Bashiru aliwataka wana CCM kutokuwa na hofu na kwamba watembee kifua mbele kutokana na kazi iliyofanywa na Serikali.

Alisema sababu na misingi ya kujivunia ushindi kwa chama hicho ni mvuto kilichonacho kwa Watanzania na kukubalika kutokana na utekelezwaji wa mambo mbalimbali ambayo hayajawahi kufanyika kabla ya hapo.

Dk. Bashiru alisema CCM ni chama cha wakulima na
wafanyakazi, hivyo ni jukumu lake kuhakikisha makundi hayo mawili yanapata yalichokitarajia.

Alitaka wakulima na wafanyakazi wa nchi hii wasibughuziwe na kwamba chama hicho hakitakubaliana na kiongozi yeyote atakayekwenda kinyume na maelekezo hayo.

Katika hatua nyingine, Dk. Bashiru aliwaagiza viongozi wa chama hicho kutowarejesha madiwani na wabunge ambao hawakufanya vizuri kwenye uongozi wao.

Dk. Bashiru alisema chama hicho kiliomba ridhaa kwa wananchi kikitangaza ilani yake na viongozi wakapewa nafasi na kila aliyeahidi na hakutekeleza asipewe nafasi tena.

Aidha pia alivishauri vyama vya siasa kutambua kuwa uchaguzi siyo kama mchezo wa bahati nasibu na wala siyo namba kama wanavyojidanganya, na kwamba kilichowapiga uchaguzi 2015 ndicho kitakachowachapa 2020.

 Alisema CCM wanapoahidi wanatekeleza na wasipotekeleza ni lazima watoe maelezo kwanini hawakutekeleza, na mwaka huu ni wa kueleza umma kwa yale ambayo hayakutekelezwa vizuri.

Alitaja mambo mawili ambayo hayakufanya vizuri kuwa ni Serikali za mitaa kutokana na baadhi ya maeneo kuwa na watendaji dhaifu katika ushiriki wao.

Dk. Bashiru alisema pia kukosa diwani mzuri, mkuu wa wilaya mzuri na mkuu wa mkoa ambao badala ya kukaa vikao kujadili changamoto za wananchi wanafikilia posho pekee.

Alisema baadhi ya halmashauri kuwa na migogoro isiyoisha na kwamba wakati huu nchi nzima viongozi wa chama lazima wajipange kwa kuwa kutokana na mvuto wa chama hicho kuna wagombea wengi wazuri watakuja kugombea.

Hata hivyo aliwataka viongozi wa chama hicho kuwapitisha wagombea waliofanya vizuri hata kwa miaka mia kwa kuwa chama hicho kina wajibu wa kushughulika na matatizo ya wananchi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles