31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Diamond, Lady Jaydee wanyakua tuzo za kimataifa

Lady Jaydee
Mwanamuziki Lady Jaydee

NA ZAINAB IDDY, DAR ES SALAAM

MSANII wa muziki wa kizazi kipya nchini anayetamba na wimbo wake wa Mdogomdogo, Nasseb Abdul ‘Diamond Platinumz’,  juzi ametwaa tuzo mbili katika tuzo za Afrika Music Magazine Award ‘AFRIMMA 2014’ kupitia kipengele cha mwanamuziki bora wa kiume Afrika Mashariki zilizofanyika Eisemann Center Richardson, Texas, Marekani.

Mkali huyo wa wimbo wa My Number One, alishinda tuzo hizo ikiwemo ya Msanii bora wa Afrika Mashariki na ile ya Wimbo bora wa kushirikiana aliofanya na msanii Davido wa Nigeria.

Katika tuzo ya Msanii bora wa kiume wa Afrika Mashariki, Diamond aliwashinda Ben Pol wa Tanzania, Bebe Cool wa Uganda, Wyre wa Kenya, Jackie Gosee wa Ethiopia na Navio wa Uganda.

Diamond aliibuka kidedea katika Wimbo bora wa kushirikiana akiwabwaga  T Pain na 2 Face – rainbow, Khona ya Uhuru na Mafikizolo wa Afrika Kusini, Surulere remix ya Dr Sid wa Nigeria, Amani aliyewashirikisha Waganda Radio na Weasel ‘Kiboko changu’, J Martins akimshirikisha Dj Arafat ‘Touching body’ na Rebees na Wizkid ‘Slow down’.

Katika tuzo hizo pia msanii mwingine wa Tanzania, Judith Wambura ‘Lady Jaydee’ alitwaa tuzo ya Msanii bora wa kike Afrika Mashariki aliyewabwaga Aster Aweke wa Ethiopia, Rema wa Uganda, Avril wa Kenya, Victoria Kimani wa Kenya na Irene Ntale wa Uganda.

Naye Mtanzania Sheddy Clever alinyakua tuzo ya Prodyuza bora baada ya kuwashinda Don Jazzy wa Nigeria, Dj Oskido wa Afrika Kusini, Shizz wa Nigeria, Killbeatz wa Ghana, Oskido wa Afrika Kusini, Nash Wonder wa Uganda na Ogopa wa Kenya.

Tuzo ya Mtayarishaji bora wa video ilinyakuliwa na Ogopa Dj’s ambao ndio waliofanya video ya ‘My number One′ ya Diamond Platnumz.

Diamond akizungumzia ushindi huo kupitia ukurasa wake wa Instagram, alimshukuru Mungu kwa kumwezesha kupata tuzo hizo.

“Kwanza ya yote napenda nimshukuru sana Mwenyezi Mungu, mama, familia, na Management, kipenzi changu, Media, bila kuwasahau nyinyi mashabiki wangu wapendwa kwani siku zote mmekuwa mkinisapoti bega kwa bega kwenye shida na raha…., Niwashukuru wasanii wenzangu toka ndani na nje kwani naamini changamoto tunazopeana ndio zimefanya hadi sasa muziki ufike hapa…hakika tuzo hizi si zangu bali ni za muziki wa Bongo fleva. Mwisho kabisa nimshukuru Rais Jakaya Mrisho Kikwete kwa mchango wake wa kila siku katika sanaa yetu!,,,Mr President your Son Did it !!!!!!

Kwa upande wake Lady Jaydee aliandika:

“Nashukuru wote mnaokubali kazi zangu, wote mnaosimama na kumtetea JayDee bila kusita, nashukuru kwa tuzo nyingine tena toka AFRIMMA. Wahenga walinena kuwa utavuna ulichopanda, mapenzi tele kwa kila mtu.

Baaadhi ya wasanii walimpongeza Diamond kwa ushindi huo, akiwemo mpenzi wake, Wema Sepetu.

Wengine waliompongeza Diamond kwa hatua hiyo ni msanii Linah Sanga, Aunt Ezekiel, Duly Sykes, Mwana FA, Linex na wengineo.

- Advertisement -

Related Articles

1 COMMENT

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles