27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Desk and Chair lawakumbuka wafungwa Butimba

*Latoa msaada wa godoro 430 yenye thamani ya Sh milioni 20.2

Na Clara Matimo, Mwanza

Katika kuendelea kuhakikisha kwamba Watanzania walio magerezani wakitumikia vifungo vyao wanaishi na kulala kwenye mazingira bora, Shirika la Desk and Chair Foundation lenye makao yake  Mkoani Mwanza limetoa msaada wa magodoro 430 yenye thamani ya zaidi ya Sh milioni 20.2 kusaidia wafungwa wa gereza la Butimba lililopo jijini hapa.

Baadhi ya viongozi wa jeshi la magereza Mkoa wa Mwanza  wakiwa katika picha ya pamoja na  Mkuu wa Mkoa huo katika gereza kuu la butimba baada ya kukabidhiwa msaada wa magodoro 430 kutoka Taasisi ya Desk and Chair Foundation leo Mei 6,2022.

Akizungumza leo Mei 6, mwaka huu wakati akimkabidhi, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Mhandisi Robert Gabriel, magodoro hayo  katika gereza hilo, Mwenyekiti wa Taasisi hiyo Tawi la Tanzania, Alhaji  Sibtain Meghjee, amesema msaada huo umetolewa na waislamu wa dhehebu la Shia ikiwa ni sehemu ya zaka wanazozitoa kwa watu na makundi mbalimbali yenye uhitaji.

Alhaji Meghjee amesema taasisi yake itaendelea  kutatua chhangamoto mbalimbali katika gereza hilo huku akibainisha kwamba  ndani ya wiki mbili kuanzia leo wataanza kufanya utafiti ili kubaini eneo ambalo maji yanaweza kupatikana  waweze kuchimba kisima kirefu gerezani hapo lengo ni  kusaidia changamoto ya upatikanaji wa maji na kupunguza gharama za kupata huduma hiyo kutoka Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira jijini Mwanza (Mwauwasa).

“Tunatarajia kuchimba kisima kirefu  ambacho kitatosheleza mahitaji ya maji katika gereza hili ingawa nimeanza kupata maombi kwenye maeneo mengine kutoka makundi mbalimbali ndani na nje ya mkoa huu lakini tutahakikisha changamoto ya maji  kwenye gereza hili  inakwisha ,”amesema Alhaji Meghjee na kuongeza

“Msaada huu tulioutoa leo umefanya idadi ya magodoro tuliyoyatoa gerezani hapa kufikia 1000 yenye thamani ya Sh milioni 47  kama  mnavyokumbuka Aprili 25 mwaka huu tulitoa msaada wa magodoro 570 yenye thamani ya Sh milioni  27, tunafurahi kukamilisha idadi hii maana ombi la Mkuu wa Magereza Mkoa wa Mwanza, Kamishna Msaidizi wa Magereza, Lazaro Nyanga, alisema anaupungufu wa magodoro 1,000,”amefafanua Alhaji Meghjee.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza,  Mhandisi Robert Gabriel,  ameishukuru na kuipongeza taasisi ya Desk anda Chair Foundation kwa  kuisaidia serikali kutoa vifaa hivyo vya kulalia maana vitawasaidia wafungwa kuwakinga na baridi pamoja na magonjwa.

“Hakuna serikali yoyote inayoweza kutosheleza kwenye maeneo yote ndiyo maana kuna taasisi, makampuni na watu binafsi wanatoa misaada kwenye jamii  ili kuisaidia ukigusa hapa kwa wafungwa umegusa umma mkubwa wa jamii, changamoto za hapa bado ni nyingi, godoro umetatua, maji pia umetuahidi matumaini yangu utaendelea kushirikiana nasi kutatua changamoto zingine zilizopo.

Mimi  naamini Mungu ameamua kukutumia wewe mzee Meghjee bila kujijua uwe ni malaika wa pekee wa kusaidia changamaoto za gereza hili la Butimba pamoja na wengine watakao kuunga mkono,  kanuni ya Mungu ni kumbariki anae toa ndiyo maana wanaotoa kupitia taasisi yenu Mungu anazidi kuwabariki na wao wanazidi kutoa, unapotoa unazidi kubarikiwa hapa hapa duniani, “amesema na kuongeza .

Sura ya Mwenyezi Mungu imejificha kwa mtu mnyonge, mhitaji na mdadifu,  ukikutana na mtu huyo umekutana na sura ya Mwenyezi Mungu, kupitia kiumbe huyo, tunapowahudumia wahitaji tunatengeneza kesho yetu njema na Mwenyezi Mungu, tunatengeneza pepo iliyo salama na hicho ndicho mlichokifanya Desk and Chair Foundation.

Mkuu wa Magereza Mkoa wa Mwanza, Kamishna Msaidizi wa Magereza, Lazaro Nyanga, amesema: “Mahitaji yetu makubwa ilikuwa ni magodoro na mlituahidi magodoro 1,000 ambayo leo mmekamilisha ahadi yenu tunashukuru sana, msituchoke sisi kama taasisi tutaendelea kuwasumbua lakini endeleeni  kusaidia jamii iliyoko gerezani, taasisi na nchi yetu kwa ujumla wake,” amesema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles