26.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

DC Misenyi: Wananchi toeni ushirikiano kwa TRA

MWANDISHI WETU- KAGERA

MKUU wa Wilaya ya Misenyi Mkoa wa Kagera, Kanali Dennis Mwila amesema ulipaji kodi ndio maendeleo ya taasisi au jumuiya yoyote hivyo wananchi wasiwaogope maafisa wa Mamlaka ya Mapato na badala yake wanatakiwa kuwapa ushirikiano.

Hayo aliyazungumza jana ofisini kwake wilayani Misenye alipotembelewa na maofisa wa TRA kutoka makao makuu waliofika mkoani Kagera kwaajili ya kuendesha kampeni ya elimu ya kodi.

Alisema wanachi wengi wanaoishi maeneo ya mpakani wamezoea kufanya biashara za magendo ambazo hazina tija kwa nchi na kwamba wanatakiwa kupewa elimu ili waweze kutambua faida na umuhimu wa kulipa kodi.

“Sisi tuliopo mpakani tuna tatizo moja la wananchi wetu wengi wamezoea kufanya magendo ambayo hayana tija na kwamba tunahitaji barabara, maji huduma nzuri za afya lakini pia hivi sasa nchi yetu inatoa elimu kuanzia awali hadi kidato cha sita na kwa wale wasiojiweza kwenda chuo kikuu wanapewa mikopo nah ii yote ni kwa sababu ya mapato,” alisema Kanali Mwila.

Alisema TRA inafanya kazi nzuri ya kutoa elimu ya kodi ambayo itamjengea mlipakodi utayari wa kulipa kodi kwa hiyari hivyo wananchi wanatakiwa kulipa kodi kwa maendeleo ya nchi.

Naye Meneja wa TRA mkao wa Kagera Adam Ntoga alisema kuwa lengo la kampeni hiyo ya elimu kwa mlipakodi ni ili kuweza kupeleka elimu hiyo kwa kila mlipakodi na kuweza kukusanya kodi ya serikali

Alisema mkoa wa Kagera una Wilaya tano zenye ofisi za TRA na kwamba hivi sasa wanafanya kufungua ofisi nyingine katika wilaya ya Kyerwa ambayo inachangia mapato katika wilaya ya Karagwe

“Tunaomba wananchi wa Kagera wajitokeze kwa wingi katika kampeni hii ya elimu ya kodi inayoendelea ili waweze kuuliza maswali pamoja na kutoa changamoto zao wanazokutana nazo ili waweze kusaidiwa,” alisema Ntoga.

Abdallah Kagoro ambaye ni mfanyabiashara katika maeneo ya mpaka wa Mtukula alisema kampeni hii ya kuwafata wafanyabiashara katika maeneo yao ya kazi ni nzuri na kwamba ingekuwa endelevu maana wanapofika katika maendeo ya kazi wanaweza kuona changamoto wanazokutana nazo.

“Wanapokuja huku kwenye maeneo yetu wanaona ni jinsi gani ambayo tunakaa bila kazi hivyo ni rahisi kwa wao kutukadiria kodi halali tofauti na wakitukadiria wakiwa ofisini.

“Nchi ni yetu sote hivyo tunatakiwa kuwa wazalendo tulipe kodi lakini tulipe kulingana na hali ya biashara na sio kulipa pesa iliyopangwa  wakati siku nyingine biashara inakuwa ngumu.” Alisema Kagoro.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles