25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

DC awataka wananchi kuandamana kuelekea mashambani

Francis Godwin, Iringa

MKUU wa Wilaya ya Kilolo, Asia Abdallah amewataa wananchi wa wilaya hiyo kujikita zaidi katika maandamano ya shambani na katika shughuli za kimaendeleo badala ya kuwasikiliza waliokuwa wagombea wa nafasi mbalimbali wanaowaza kuvuruga amani kwa kutamani maandamano yasiyo na tija ya kiuchumi .

Mkuu huyo wa wilaya alisema jana kuwa wananchi wanapaswa kutambua kuwa muda wa kampeni kwa  ajili ya  kupata  viongozi  watakaowatumikia kwa  kipindi cha miaka mitano umekwisha pita na  sasa  ni wakati wa  wananchi pamoja na  viongozi hao kufanya kazi .

Hivyo alisema itakuwa si sawa kwa mwananchi wa Kilolo kuacha kufanya shughuli za  kimaendeleo na kushughulishwa na maandamano yasiyo na tija katika ustawi wa maisha yao.

“Tunahitaji kuona wanasiasa sasa wanashiriki katika ujenzi wa Taifa kwa kuhamasisha  wananchi kufanya maandamano ya wananchi kujishughulisha na shughuli za kimaendeleo  kuliko kuhamasisha wananchi kwenda  barabarani kuandamana ama kushinda vijiweni,” alisema.

Mkuu huyo wa wilaya aliwataka vijana Wilaya ya Kilolo kuwapuuza wale wote ambao  wanatamani kuona amani ya nchi hii inavurugwa kwa kutamani maandamano na vurugu badala yake anatamani kuona kila kijana anajishughulisha katika kazi za uzalishaji mali.

Asia alisema katika Wilaya ya Kilolo uchaguzi umefanyika katika hali ya amani na utulivu mkubwa na kuwapongeza wananchi kwa  kutimiza wajibu wao wa kikatiba kwa amani na utulivu, pia kuwapongeza wale ambao wamechaguliwa kuwa viongozi akiwemo Rais Dk. John  Magufuli, mbunge wa Kilolo, Justin Nyamoga na madiwani wote waliochaguliwa.

Aidha, aliwataka wazazi wilayani humo kuendelea na maandalizi ya kuwapeleka watoto wao shule hapo mwakani kwa kuwa ni jukumu la kila mzazi ama mlezi kuhakikisha mtoto wake anapata elimu na anasimamiwa vema ili kupata elimu hiyo mwanzo hadi mwisho, bila  kukatishwa masomo ama mzazi kumgeuza mtoto  huyo kuwa ni  sehemu ya watafutaji wa fedha za familia.

Alisema  kwa wale watoto waliohitimu elimu ya msingi wazazi kuendelea kuwalea kwa   kuwalinda watoto hao ili wasirubuniwe na mtu yeyote kwenda mijini kufanya kazi za ndani ama kupewa mimba kwa wale wa kike.

“Serikali hii chini ya Rais John Magufuli imeendelea kuboresha mazingira bora ya elimu kwa  kuondoa changamoto mbali mbali katika elimu hata kuamua kufuta ada kwa elimu msingi ” alisema.

Hivyo  alisema jukumu la mzazi na mlezi ni kusimamia watoto kwenda shule na kuwalinda na vikwazo ambazo vinaweza kuwavurugia masomo yao na sio wasimamizi hao wa mtoto kuwa  chanzo cha kuwaharibia maisha watoto hao kutofikia ndoto za serikali za elimu bora.

Asia alisema Serikali haitaacha kuwachukulia hatua wazazi ama walezi ambao watabainika   kuwakwamisha watoto  wanaopaswa kwenda  sekondari ama kupata elimu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles