NA FRANCIS GODWIN- IRINGA
MKUU wa Wilaya ya Kilolo mkoani Iringa, Asia Abdalah, amepiga marufuku wanafunzi wa shule za msingi wilayani humo kujipikia chakula wakati wa masomo .
Alikuwa akizungumza jana na walimu na kamati ya Shule ya Msingi Mlowa Kata ya Mahenge wakati wa ziara yake ya kukagua miundombinu ya shule.
Alisema hajapendezwa na utaratibu wa shule hiyo wa kuwaacha wanafunzi kuingia jikoni kujiandalia chakula cha mchana badala ya kujisomea.
DC aliagiza kamati ya shule hiyo na shule nyingine zote wilayani Kilolo kutafuta wapishi watakaofanya kazi ya kuwaandalia chakula wanafunzi hao.
Alisisitiza kuwa asingependa kuona wanafunzi wakiacha masomo na kuingia jikoni kupika chakula.
"Sijapendezwa hata kidogo kuona wanafunzi wanapika chakula badala ya kusoma, naagiza kuanzia leo shule zote kutafuta wapishi wa kuwahudumia wanafunzi hao.
“Sitegemei kuona tena wanafunzi wanajipikia chakula….natoa muda hadi Jumatatu wiki ijayo iwe mwisho,”alisema.
Hata hivyo, DC alipongeza jitihada mbalimbali zinazofanywa na kamati ya shule hiyo kwa kukamilisha vyumba viwili vya madarasa na kuwaepusha wanafunzi waliokuwa wakisomea chini ya mti kuanza kusomea darasani.