25 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Dawa mpya ya Ukimwi kuleta faraja kwa wenzi

prep-400x210Mwandishi Wetu na Mashirika ya Habari

UTAFITI mpya wa ugonjwa wa Virusi vya Ukimwi (VVU), unatarajiwa kuleta faraja kwa wenzi, ambapo mmoja anaishi na virusi hivyo na mwingine akiwa hana.

Faraja hiyo inahusisha kufanya tendo la ndoa bila kutumia kinga na hivyo kupata watoto bila kusababisha maambukizo yoyote mapya baada ya unywaji wa dawa.

Ugunduzi wa dawa hiyo mseto ya kimiminika ijulikanayo kama PrEP, tayari imetumiwa na wanaume mashoga nchini Uingereza na Marekani.

Dawa hiyo huweza kuondoa hatari ya kuambukizwa hadi asilimia sifuri, itaondoa changamoto iliyokuwapo katika njia namba moja ya kujikinga na virusi, yaani kutumia kondom wakati wa kufanya tendo la ndoa.

Matumizi ya kondom yalimaanisha kuwa wenzi wa aina hiyo hawawezi kupata watoto bila uwezekano wa kuhatarisha mwenzi ambaye hana VVU.

Kwa sababu hiyo, mamlaka nchini Kenya zimeanzisha mradi wa kuwasaidia wenzi kuwa na familia bila kuhatarisha afya zao.

 

Kenya

John na mkewe Josephine, wanaoishi kaskazini mwa Nairobi ni mfano wa wenzi wa aina hiyo, ambapo  Josephine anaishi na VVU wakati John hana maambukizo hayo.

Mume huyu anasema kuwa hali kama hiyo inaweza kuwa ngumu na anawajua wenzi ambao wameshatengana kwa sababu hiyo.

Kuna wenzi 260,000 nchini Kenya, ambako mmoja anaishi kwa VVU huku mwenzake akiwa hana.

Wenzi wa aina hiyo wanaojulikana kitaalamu kama serodiscordant, wanachukua asilimia 44 ya mambukizo mapya ya VVU katika taifa hilo. Pamoja na asilimia hiyo  wamezaa watoto.

“Lakini nia ya kupata watoto kwa wenzi wa aina hii bado huwa na nguvu mno –utafiti mmoja wa hivi karibuni kwa wenzi wa serodiscordant umeonesha asilimia 17 ya wanawake walipata mimba.

“Kwa sasa majaribio mapya ya dawa yametoa mwanga wa matumaini na faraja kwa wenzi wa aina hii,” anasema John.

Imebainika kwamba njia mpya ya kutumia dawa za kukabiliana na VVU, ambazo kwa kawaida hupewa watu wanaoishi na virusi hivyo, inaweza kutumika kwa wenzi wa aina hiyo kujaribu kuzaa watoto wasio na VVU bila pia kumwambukiza mwezi asiye na virusi hivyo.

Dk. Mugo

Dk. Nelly Mugo kutoka Taasisi ya Utafiti wa Tiba ya Kenya na timu ya wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Washington cha nchini Marekani kwa pamoja wanaendesha majaribio hayo.

Majaribio hayo yalihusisha wenzi  4,700, ambao mmoja ana VVU na mwingine hana maambukizo.

Katika majaribio hayo, mtu ambaye hakuambukizwa VVU alikunywa PrEP katika kipindi cha miezi 36.

“Tulibaini kwamba kuwa na dawa katika mfumo wako mwilini kulipunguza kiwango cha maambukizo kwa zaidi ya asilimia 90.

“Lakini pia iwapo mwenzi mwenye VVU pia alichukua dawa za kufubaza makali ya Ukimwi (ARVs), uambukizo wa VVU ulipunguzwa hadi asilimia sifuri au karibu na sifuri,” alisema.

Katika baadhi ya jamii shinikizo la kijamii la kutaka kuwa na watoto linaweza kuwa kubwa huku familia zisizo na watoto mara nyingi zikipata shida kueleza kwanini hazijazaa.

Katika utafiti wa karibuni, wenzi walieleza kwamba walijisikia kutokuwa na la kufanya na wako katika hatari ya kupata VVU iwapo watajaribu kupata mimba.

Lakini katika mradi wa sasa, wenzi wasioambukizwa walipata faraja baada ya kubakia salama bila kuambukizwa walipofanya tendo la ndoa bila kinga, hali iliyosababisha imani kwa dawa hiyo kuwa na uwezo wa kuwalinda.

Dk. Mugo anasema: “Hisia za kawaida zilizozoeleka kwa kuzaa watoto ni pamoja na kutimiza matarajio ya wenzi husika ya ukubwa wa familia waitakayo, kupata watoto wao wenyewe wa kuwazaa na kuendeleza uhusiano imara na mara nyingi muhimu zaidi ikiwa ni kukabiliana na shinikizo la nje kutoka kwa jamii” alisema.

VVU haitibiki, kwa sababu mara inapoingia katika mwili, hujificha katika mahali ambapo ni vigumu kupafikia, na kusababisha hodhi, hali inayomanisha kwamba kamwe haiwezi kuondolewa kutoka humo hodhini.

Nadharia iliyo nyuma ya PrEP ni kwamba kuchukua dawa za ARVs kabla ya kuambukizwa kunamaanisha tayari zipo ndani ya mwili.

Lakini watafiti wameonesha kuwa iwapo mtu asiyeambukizwa tayari atakuwa na dawa za PrEP katika mifumo yao ya mwili wakati virusi vinapoingia katika miili yao hiyo huuawa.

Hili linamaanisha kuwa virusi huwa havina nafasi ya kujificha katika hodhi, na hivyo ni vigumu kwa mtu kuambukizwa.

“PrEP ni kitu kizuri kinachoweza kuwafaa wenzi hawa,” anasema Dk. Mugo, kwa sababu inaweza kutatua kile alichokiita ‘hali tete ya ufarakano.

“Wakati unapobaini mwenzi wako ana VVU husababisha maumivu makubwa ya kihisia,” aliongeza. “Lakini uhusiano na hisia na mapenzi vina nguvu kuliko virusi.

“Wengi wa wenzi hutaka kubakia pamoja, lakini wanashindwa kurejea katika hali ya kawaida ya uhusiano wa tendo la ndoa. PrEP ina uwezo mkubwa wa kutatua tatizo hilo,” anasema.

Jaribio hilo lilikuwa na mafanikio kwani kufikia Septemba 2015, Shirika la Afya Duniani (WHO) lilipendekeza kuwa watu walio katika hatari ya kupata VVU wapatiwe PrEP kama chaguo la pili la kujikinga, kama sehemu ya uzuiaji wa maambukizo.

 

Bodi ya Afya ya Kenya kwa sasa inafikiria kutoa kibali kwa dawa hiyo kusambazwa kwa wenzi, ambao mmoja wapo ana VVU mwingine akiwa hana nchini humo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles