26.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

CUF MAALIM YAKWAMA MAHAKAMANI

Na Kulwa Mzee-Dar es Salaam


MAOMBI ya kuwazuia Mbunge wa Kaliua, Magdalena Sakaya(CUF), Mbunge wa Mtwara Mjini, Maftah Nachuma(CUF) na wenzao sita kujihusisha katika masuala ya uongozi na kufanya mikutano ya chama hicho yamegonga mwamba kwa sababu waliofungua walisema uongo.

Maombi hayo yalitupwa na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu. Wilbroad Mashauri baada ya kubaini kwamba CUF haina Bodi ya Wadhamini hivyo aliyeapa alisema uongo.

Katika maombi hayo wadai ni Bodi ya Wadhamini wa CUF waliokuwa wakiwakilishwa na Wakili Hashimu Mziray na wadaiwa ni Sakaya, Nachuma, Thomas Malima, Omar Masoud, Abdul Kambaya, Salama Masoud, Zainabu Mndolwa na Jaffari Mneke waliokuwa wakiwakilishwa na Wakili Mashaka Ngole.

Wakili wa wadaiwa, Ngole aliwasilisha majibu ya kiapo kinzani kilichoapwa na wajibu maombi wote nane pamoja na pingamizi la awali dhidi ya maombi yaliyopo mahakamani.

Alidai anapinga maombi hayo namba 45/2017 kwa kuwa hayawezi kusikilizwa katika mahakama hiyo kwasababu yanashughulikiwa katika maombi namba 23/2016 yaliyopo Mahakama Kuu.

Anadai mwombaji hana miguu ya kusimamia kufungua kesi dhidi ya wajibu maombi, maombi hayo hayana msingi kwa kushindwa kubainisha jina la mwandishi wa masuala ya fedha hivyo waliiomba mahakama kuyatupilia mbali maombi hayo kwa gharama.

Pia wadai walipinga Joram Bashange kuwa hana sifa za kuapa kama Katibu wa Bodi ya Wadhamini ya CUF kwa vile nafasi yake ya ukatibu ilikoma tangu Oktoba mwaka jana.

 Akitoa uamuazi Hakimu Mashauri alisema kwa kuwa maombi kama hayo yako Mahakama Kuu, maombi yaliyopo katika mahakama ya chini lazima yasimame ili ya kwanza yapite.

“Mahakama ilitilia maanani taarifa ya Wakala wa Vizazi na Vifo (RITA), ambao ni wasajili kwamba hadi sasa haijasajili bodi ya wadhamini ya chama hicho na kwamba pande zote mbili zinazopingana zilipeleka maombi ya usajili Rita.

“Rita haijasema chochote kuhusu bodi, aliyesema kuna bodi ya wadhamini ni uongo, kiapo ni ushahidi mahakamani, haiwezi kusikilizwa kesi kwa kiapo cha uongo, mahakama inatupilia mbali maombi ya zuio la muda,  Joram Bashange wa Bodi ya Wadhamini atabeba gharama za kesi,”alisema.

Awali Wakili wa Bodi ya Wadhamini, Hashim Mziray aliwasilisha maombi madogo chini ya hati ya dharura, akiomba mahakama iwazuie kwa muda wajibu maombi kujihusisha katika masuala ya uongozi na kufanya mikutano ya chama.

Bodi ya wadhamini inaomba mahakama itoe zuio la muda kuwazuia wajibu maombi, mawakala wao au watu wao wowote kujihusisha katika masuala yoyote ya uongozi au kufanya mikutano ya chama hicho, hadi maombi yao hayo yatakaposikilizwa kwa pande zote husika.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles