25 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

CUF kuandamana kupinga uchaguzi wa marudio Z’bar

severinaNA SHABANI MATUTU, DAR ES SALAAM

JUMUIYA ya Wanawake ya Chama cha Wananchi CUF (JUKECUF), inatarajia kuongoza maandamano Februari 22, jijini Dar es Salaam, kuunga mkono hatua ya chama hicho kutoshiriki uchaguzi wa marudio Zanzibar.

Maandamano hayo yatashirikisha wanawake wa chama hicho na wananchi wengine wenye mapenzi mema na chama hicho cha upinzani.

Akisoma tamko la uamuzi huo, Mwenyekiti wa JUKECUF, Severina Mwijage, alisema jumuiya hiyo itafanya maandamano ya kuunga mkono uamuzi wa Baraza Kuu Taifa la chama hicho wa kutoshiriki uchaguzi huo wa marudio kwa sababu Uchaguzi Mkuu ulikwishafanyika na chama hicho kilishinda.

“Maandamano hayo yanatarajiwa kufanyika Februari 22 kuanzia saa 4 asubuhi yakishirikisha akina mama na wananchi mbalimbali, wapenda demokrasia na amani,” alisema Severina.

Mwenyekiti huyo ambaye pia ni mbunge wa viti maalumu, alisema maandamano hayo yataanzia katika Ofisi Kuu ya CUF, Buguruni kuelekea Ofisi ya Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan.

“Maandamano hayo yatapita Barabara ya Uhuru, Karume, Kariakoo, Mnazi mmoja, Sokoine, Bandari, Mahakama Kuu, Mahakama ya Ardhi hadi Ofisi ya Makamu wa Rais,” alisema Severina.

Alisema sababu iliyowasukuma kufanya maandamano hayo inatokana na jumuiya hiyo kutambua kwamba amani visiwani Zanzibar ikivurugika watakaoathirika zaidi ni wanawake na watoto.

“Sisi kama wanawake wa taifa hili hatuko tayari kushuhudia wanawake na watoto wakipata tabu Zanzibar kwa ajili ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kulazimisha ushindi,” alisema Severina.

Kutokana na hilo, alisema tayari wameshatoa taarifa kwa Kamishna wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro.

Hivi karibuni, Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), Jecha Salum Jecha, alitangaza kurudiwa kwa uchaguzi Machi 20, uamuzi ambao umepingwa na vyama 10 vya upinzani, kikiwamo CUF.

Jumuiya za kimataifa pia haziungi mkono kurudiwa kwa uchaguzi huo zikidai kwamba ule wa mwanzo uliofanyika Oktoba 25 mwaka jana haukuwa na kasoro kubwa za kuufanya kuwa batili.

Kurudiwa kwa uchaguzi huo kunatokana na ZEC kufuta Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 mwaka jana, kwa madai ya kuwapo dosari mbalimbali

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles