NA SHABANI MATUTU, DAR ES SALAAM
BARAZA Kuu la Uongozi la Chama cha Wananchi (CUF), linatarajia kukutana leo jijini Dar es Salaam ili kuamua hatima ya chama hicho kushiriki ama kutoshiriki uchaguzi wa marudio visiwani Zanzibar.
Huku uchaguzi huo ukitarajiwa kufanyika Machi 20, mwaka huu jana Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, aliongoza kikao cha Kamati ya Utendaji ya Taifa ambapo pamoja na mambo mengine walijadili kuhusu uamuzi wa Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC), kutangaza tarehe ya uchaguzi huo.
Taarifa iliyotolewa jana jijini Dar es Salaam na Ofisa Habari wa chama hicho, Silas Bwire, ilieleza kwamba kikao hicho cha Kamati ya Utendaji kilikuwa na kazi ya kuandaa ajenda za kikao cha Baraza Kuu la Uongozi kitakaa kwa ajili ya uamuzi.
“Jukumu kubwa la kikao cha Kamati ya Utendaji kwa mujibu wa sheria ni kuandaa ajenda kwa ajili ya kikao cha Baraza Kuu litakaloanza kesho (leo). Kamati tendaji ina wajumbe wapatao 18 kutoka bara na visiwani ambao ni viongozi waandamizi wa chama na mwenyekikti wa kikao hicho ni katibu mkuu wa chama.
“Baraza Kuu lenye wajumbe wapatao 60 kutoka sehemu mbalimbali Tanzania litajadili kwa kina ajenda zitakazopelekwa na kikao cha kamati tendaji kisha kufanya maamuzi,” alisema Bwire.