25.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Corona yatikisa Pasaka, wafanyabiashara walia

Na AVELINE KITOMARY -DAR ES SALAAM 

BAADHI ya wafanyabiashara katika jiji la Dar es Salaam wamesema mlipuko wa homa kali ya mapafu inayosababishwa na virusi vya corona (Covid-19) umesababisha kukosa wateja kipindi hiki cha msimu wa Sikukuu ya Pasaka.

MTANZANIA Jumapili lililopita maeneo mbalimbali ya manunuzi ikiwemo Soko Kuu la Kariakoo lilibaini idadi ndogo ya watu ikilinganishwa na msimu wa sikukuu nyingine.

Akibainisha hali ilivyo, mmoja wa wafanyabiashara wa nguo katika Soko la Kariakoo, James Mboja alisema tangu kuanza kwa mlipuko huo nchini China, mzunguko wa biashara umekuwa mdogo kutokana na upatikanaji mdogo wa bidhaa.

“Sio hilo tu hata hapa ndani bado wateja hawaji wengi kununua, ukiwauliza wanakwambia hatuna hela, hasa kipindi cha corona ilivyotangazwa nchini ndio kabisa watu wanalalamika hawana hela ya kununua vitu.

“Kipindi cha sikukuu za nyuma dada yangu nikwambie tu Kariakoo kupitisha hata mguu ni shida, lakini sasa hivi unaona kabisa watu wamepungua, unapita kwa uhuru hapa.

“Ukizingatia bei ya bidhaa ni ile ile, hatujapandisha bei nguo, mfano shati nauza 7,000 lakini sasa hivi mteja akiongea vizuri hata 5,000 namwachia, hali ya biashara ni ngumu,” alifafanua Mboja.

Hasan Thabiti, mfanyabiashara wa viungo, alikiri pia kuwepo kwa hali mbaya ya biashara kutokana na kupata idadi ndogo ya wateja.

“Nafikiri kinachosababisha tusipate wateja ni kwamba watu hawana hela, idadi ya watu wanaokuja mjini imepungua  kutokana na kutokuwa na fedha, nilitegemea kwa wakati huu ndio tungepata fedha, lakini kipindi hiki mambo yamebadilika,” alieleza Thabiti.

Naye Juma Ally, mfnyabiashara wa mchele katika soko la Mapinduzi Mwananyamala, alisema wateja anaowapata ni wale wa siku zote na hadi jana hakuna ongezeko la wateja.

“Katika kipindi cha sikukuu kama hii huwa tunauza sana kutokana na ongezeko la wateja, lakini kwa sasa hakuna ongezeko na biashara imeshuka tangu corona ianze.

“Nilikuwa na uwezo wa kuingiza hata Sh milioni 1 kwa siku, lakini sasa hivi napata Sh 50,000 hadi 20,000 siku nyingine, yaani sikufichi hiyo ‘gap’ (pengo) ni kubwa mno.

“Hatujapandisha bei ya mchele hapa, ni kuanzia Sh 1,500 hadi 2,000 hii ndio siku zote tunauza, sasa hata kama ukipandisha unampandishia nani wakati wateja hawapo, yaani hapa nafikiria kupunguza zaidi ili kuvutia wateja,” alisema Ally. 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles