27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Corona yaathiri sekta ya uwindaji nchini

Na RAMADHAN HASSAN-DODOMA

SERIKALI inatafakari namna ya kusaidia sekta ya uwindaji isiathirike zaidi katika kipindi hiki cha sakata la ugonjwa wa corona.

Hayo yalielezwa jana, jijini hapa na Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Costantino Kanyasu, alipokutana na wawakilishi wenye vitalu vya utalii nchini.

Kanyasu alikiri kuwa biashara hiyo imekuwa ngumu zaidi katika kipindi hiki hivyo kwa namna yoyote hali haiwezi kutengemaa kwa wakati mfupi na kuwapa faida wenye vitalu.

Alisema tishio la corona limekuwa na madhara katika sekta ya utalii ambapo Serikali inapaswa kutupia jicho kwa wazawa waliowekeza mitaji yao kwenye vitalu.

Hata hivyo alisema ombi la kuwaondolewa kodi za vitalu linaweza kuwa gumu kutokana na kuwa lipo kisheria, lakini kwa upande wa tozo ambazo zipo chini ya Waziri wa Maliasili, jambo hilo ni muhimu kuwasaidia.

“Mimi mwenyewe hivi karibuni nilitembelea baadhi ya hoteli ambazo zinaweza kulaza hadi watu 100, lakini nilikuta wapo watano hadi sita kwa baadhi maeneo kwa hiyo wanachokisema wako sahihi,” alisema Kanyasu.

Mwenyekiti wa Chama cha Wawindaji Nchini (TAHOA), Michel Mantheakis alisema hali ilikuwa mbaya kwa zaidi ya miaka 10 iliyopita lakini kwa sasa imekuwa mbaya zaidi kutokana na corona.

Michel alisema wageni wengi wameamua kuahirisha safari zao na baadhi wametoa taarifa kuwa watakuja mwakani huku wengine wakidai kurudishiwa fedha walizokuwa wametanguliza kwa madai watajipanga upya hali ikitulia jambo alilosema ni hatari kwa sekta ya utalii.

Mwenyekiti huyo alisema kiwango cha fedha kinachopotea katika sekta hiyo ni kikubwa kwani Tanzania ingeingiza dolla 200,000 hadi 300,000 kwa kuwinda asilimia mbili tu ya wanyama wenye sifa za kuwindwa.

Makamu Mwenyekiti wa Tahoa, Hilali Diffi alisema wanapitia katika kipindi kigumu kwa sasa lakini wanaamin Serikali ikiwasikiliza watavuka salama.

Diffi alisema moja ya mapendekezo yao kwa Serikali ni kuongezewa muda wa siku 60 katika vitalu ambavyo walitakiwa kuvirudisha machi 30 badala yake wapewe muda wa hadi Mei 30 kabla ya kuvirudisha au kuhuisha.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles