27.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 18, 2024

Contact us: [email protected]

Chui aingia ndani ya nyumba atoweka na mtoto

SAMWEL MWANGA,MASWA.

MTOTO wa miaka mitano, Masunga Milekwa mkazi wa Kijiji cha Mlimani  Kata ya Mbaragane wilayani Maswa mkoani Simiyu,  amefariki dunia baada ya kuchukuliwa na mnyama aina chui,  wakati akiwa amelala ndani ya nyumba na watoto wenzake wawili.

 Akithibitisha kutokea tukio hilo, Mkuu wa Wilaya ya Maswa, Aswege Kaminyoge alisema tukio hilo lilitokea Septemba 17, mwaka huu saa 8 usiku, baada ya mnyama huyo kutoka vichakani na kuingia ndani ya nyumba  ambayo walikuwa wamelala watoto hao  pamoja na mbuzi. 

Alisema kwa taarifa alizozipata,mnyama huyo aliingia ndani ya nyumba kwa kuangusha mlango uliokuwa wa matete na kumchukua mtoto, kisha kumburuza takribani ya umbali wa mita 200 kwenye mlima na kuanza kutenganisha kichwa na kiwiliwili.  

Akizungumza na wananchi waliokusanyika eneo tukio nyumbani kwa Magembe Buluguta, Kaminyongea  pamoja na kutoa pole kwa familia,ndugu,jamaa na wananchi wa kijiji hicho waliopatwa na msiba huo, alisema  sasa wananchi washirikiane na askari wa wanyamapori kuhakikisha wanamsaka mnyama huyo.

Alisema wakimpata mnyama huyo, wamuue na wachukue tahadhari wakati  wanamsaka,  maana baadhi ya watu wametoa ushuhuda wa kumwona wakati wanakuja kwenye msiba wa mtoto hivyo bado yuko mazingira hayo.

“Ninaomba vijana wenye nguvu katika kijiji hiki mtaungana na askari wetu wa wanyamapori kumsaka mnyama huyo ambaye ameondoa uhai wa mtoto wetu,akipatikana auawe na kwa kuwa tumepata ushuhuda kutoka kwa kina mama waliokuwa wanakuja msibani, wamemwona kila mmoja wetu achukue tahadhari maana bado yuko kwenye mazingira yetu,”alisema.

Aliwataka wananchi wa kijiji hicho kuacha tabia ya kulaza mifugo na binadamu ndani ya nyumba na kusisitiza kuwa ni lazima waimarishe milango ya nyumba zao.

Askari wa wanyamapori kutoka pori laaAkiba la Maswa lililoko mkoani hapa ambaye hakutaka jina lake liandikwe gazetini kwa kuwa si msemaji, alisema  kwa mazingira ya kijiji hicho jinsi yalivyo chui anaweza kukaa kama atapata chakula.

Alisema  kwa tabia za mnyama huyo, alikuwa anafuata harufu ya mbuzi, lakini alipoingia na kukuta watoto wamelala ndipo alipomchukua marehemu.

“Kawaida ya yule chui alikuwa anafuata harufu ya mbuzi katika harakati zake za kutafuta chakula,alipokutana na kitu ambacho anakula alichukua kile ambacho anaweza kukibeba,tusiwe na imani za kishirikina  aliwaacha watoto wengine na kuchukua yule mdogo hizi ndizo tabia za mnyama huyu,”alisema.

Alisema katika tukio hilo, Serikali itatoa kifuta machozi na siyo fidia kwa familia iliyopatwa na msiba baada ya taratibu kukamilika.

MWISHO

Wakazi 100,000 kupata huduma

 kuzuia magonjwa ya mlipuko

Na  Walter  Mguluchuma-Katavi

WAKAZI zaidi ya  100,000 wa Kata ya Majimoto  katika  Halmashauri ya Mpimbwe  wilayani Mlele, wanatarajia kusogezea huduma za matibabu ya magonjwa ya milipuko  pindi yatakapokuwa yametokea kufuatia kuanza kujengwa kwa kituo cha afya ambacho kitakuwa kinatoa matibabu yote pamoja na upasuaji .

Hayo yalisemwa hivi karibuni na Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Mpimbwe, Dk.Edward Sengo alipokuwa akitoa taarifa kwa Mkuu wa Mkoa wa Katavi,  Juma Homera   juu ya maeneleo  ya ujenzi wa kituo kipya cha afya cha Majimoto  ambacho ujenzi wake umemalizika.

Kituo hicho kinatarajia  kutoa huduma kwa wakazi z hao ambao sasa wanalazimika kutembea umbali wa kilometa 20 ili kupata huduma zinazotplewa   kwenye hospitali na  kwenye vituo vya afya .

 Alisema wananchi wa kata hiyo, walikuwa wakipatiwa huduma za  dawa za chanjo  za kuondoa na kujikinga na magonjwa mbalimbali ya milipuko  ikiwepo ugonjwa wa surua  na kuharisha  wanatarajia  kusogezewa huduma, baada ya kuanza kwa ujenzi wa kituo cha afya kitakachowasaidia kuondokana na kutembea  umbali mrefu kwa ajiri ya kupatiwa huduma  matibabu .

Alisema halmshauri hiyo kwa sasa inajumla ya vituo vya kutolea hutuma za afya 13 hospitali moja na vituo vya afya viwili hivyo kutokana na eneo la kata hiyo kuwa na idadi kubwa ya watu ndio maana wameamua kujenga kituo hicho.

Alisema idadi ya  magonjwa yakuambukiza halmashauri  yamepungua kutokana na jitihada kubwa zinazofanywa na wataalamu wa afya kufanya kazi kubwa yakuhamasisha watu kujitokeza mara kwa mara kwenye vituo  vinavyo  toa  .

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mpimbwe, Catheli ni Mashauri alisema  wananchi ambao wamekuwa wakiongezeka siku kwa siku wamekuwa wakitumia zahanati iliyopo kwenye kijiji hicho kutokana na kuwa na idadi kubwa ya watu zaidi ya laki moja zahanati hiyo kwa sasa imezidiwa na  kwa  kuhuumia idadi hiyo kubwa ya wagonjwa..

 Alisema ujenzi umeanza kwa fedha zilizotolewa na ofisi ya mkuu wa mkoa waliotowa kiasi cha milioni 45 , halmashauri ya  Mpimbwe wametowa milioni 30 wananchi wa kata hiyo nao hadi sasa wamechangia matofali yatakayo jenga kituo hicho na zaidi ya shilingi milioni nane.

 Alisema  wameanza ujenzi wa majengo ya utawala na yatakapo kamilika wataanza ujenzi wa wodi, chumba cha upasuaji na chumba cha kuhifadhi maiti  na ujenzi huo ukikamilika utawasaidia wananchi kupata huduma kwa karibu na kwa haraka hata kama magonjwa ya milipuko yatakapo tokea .

Mkuu wa Wilaya ya Mlele,  Rachael Kasanda alisema  ujenzi wa  kituo hicho kinajengwa kwa kutumia ramani za vituo vya afya vinavyojengwa sehemu mbalimbali na wanatarajia kufanya arambee za kukusanya fedha za kukamilisha ujenzi huo .

Mwisho

Upatikanaji taulo za kike

vijijini utasaidia masomo

Na Amina Omari,Mkinga

IMEELEZWA  taulo za kike (pads), iwapo zitapatikana kwa uhakika kwenye shule hasa maeneo ya vijijini, zitaongeza mahudhurio ya wanafunzi wa kike.

Hayo yalielezwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Halimashauri ya Wilaya ya Mkinga, Rashid Gembe wakati wa utambulisho wa mradi wa hedhi salama unaofadhiliwa na mtandao wa watu wanaoishi na virus vya UKIMWI SHDEPHA kwa wakuu wa idara za maendeleo ya jamii na maofisa elimu msingi na sekondari wilayani humo.

Alisema imekuwa nichangamoto kubwa kwa watoto wanaotoka familia duni kupata vifaa hivyo, hali inayosababisha kutohudhuria masomo  kwa wakati.

“Tunaamini upatikanaji wa taulo hizi katika shule zetu, utakuwa mwarobaini wa changamoto ya utoro kwa watoto wa kike, hivyo kupata fursa ya kuhudhuria masomo bila ya vikwanzo,”alisema.

Mratibu wa Mtandao huo, Marium Kamote aliziomba halmashauri kutenga bajeti ndogo kupitia mapato yao ya ndani ambayo itaweza kutumika kununua pedi kwa ajili ya kuziweka katika shule.

Alisema Serikali na jamii, vinajukumu la kuhakikisha lina mlinda mtoto wa kike kwa kuhakikisha anakuwa na hedhi salama na kumuepusha na vikwanzo vinavyomzua kutimiza lengo lake .

“Tungependa kuona halmashauri inatenga bajeti ndogo kwa ajili ya kumsaidia mtoto wa kike kuboresha mazingira yake ya kupata elimu na hedhi haiwi kikwazo cha kushindwa kufikia malengo yake”alisema.

Ofisa Mradi Hedhi Salama, Devotha Mbenna alisema  mradi unatarajiwa kuwepo wilaya tano za mkoa huo kwa ajili ya kujenga uelewa kuhusu hedhi salama.

Alisema wanatarajia elimu ya hedhi salama kufika kwa wanafunzi wa kike na wakiume ili waweze kuona hedhi ni jambo la kawaida tuu.

Mganga Mkuu wa Wilaya ya Mkinga, Dk. Joseph Ligoha alisema licha ya elimu ya uhamasishaji hedhi salama kulenga ngazi ya shule, jukumu hilo linatakiwa kuanzia ngazi ya familia.

.

Mwisho

Jukwaa la Naweza lawapa somo kina mama

Na Mwandishi Wetu- Mwanza

JUKWAA la Naweza limesema iwapo mama ataanza kumpatia vyakula mtoto ambaye hajafikisha miezi sita anaweza kumsababishia magonjwa mbalimbali.

Miongoni mwa magonjwa hayo, ni  pamoja na utapiamlo,kuharibu mfumo mzima wa makuzi yake, ni vema wakazingatia maelekezo nay a wataalamu wa afya.

Jukwaa hilo, limesema atoto wanapougua au kuonyesha dalili za kuumwa, wazazi wanapaswa kuwakimbiza hospitalini,badala ya kwenda kwa waganga wa kienyeji.

Hayo yalisemwa na wataalaamu wakati wa kongamano la afya ya mama na mtoto lilioandaliwa na Mradi wa Usaid Tulonge Afya kwa ajili ya kuwapatia elimu makuzi ya watoto wanawake Wilaya ya Nyamagana jijini Mwanza jana.

Mratibu wa Afya ya Uzazi na Mtoto wa Halmashauri ya Jiji la Mwanza, Bertha Yohana alisema kumekuwapo na changamoto ya afya ya makuzi ya watoto kutokana na mila, tabia na desturi za jamii kushindwa kuzingatia maelekezo ya wataalamu.

“Tumekuwa na tabia kwenye jamii wanafundishana wao kwa wao, wapo wanaoamini mtoto akinyonya maziwa ya mama pekee hashibi, jambo hili sio kweli, anaweza kunyonya maziwa ya mama akashiba bila kula chakula kingine mpaka afikishe miezi sita,” alisema

Alisema wakati mwanamke anapokuwa ananyonyesha mtoto mchanga, anatakiwa asiwe na msongo wa mawazo, ale ashibe ili aweze kuzalisha maziwa ya kutosha.

Mhudumu ngazi ya jamii Kata ya Mhandu, Rachael Mahulu alisema hakuna budi jamii ikaondokana na mila potofu za kuataka kuwalisha watoto wadogo vyakula na dawa kwa misingi ya kuwakuza kumbe kufanya hivyo wanawaharibu.

“Mtoto akiota meno  yanaitwa ya plastikli, wengi wanawakimbiza kwa waganga na kuwapaka dawa za kienyeji, kumfanya hivi ni kosa, nenda hospitali utapewa mwongozo,” alisema.

Ofisa Uwanda kutoka mradi wa USAID Tulonge Afya Wilaya ya Nyamgana, Esuphvat Lewis alisema katika kongamano hilo wamefundisha tabia nne za kiafya katika makuzi ya mtoto ambayo ni pamoja na unyonyeshaji wa maziwa kwa kipindi cha miezi sita.

Zingine ni kuhakikisha mama analala na mtoto kwenye chandarua kimoja angalau mpaka afikishe miezi tisa, mama akiona dalili zozote hatarishi ampeleke mtoto hospitalini na njia za uzazi wa mpango baada ya mtoto kufikisha miezi 24.

Alisema katika mafunzo hayo, wanawake 50 wameshiriki kutoka kata za Wilaya ya Nyamagana.

Baadhi ya wanawake walioshiriki mafunzo hayo, Tatu Ramadhani na Esther Suleiman kwa nyakati tofauti walisema  mafunzo hayo yameweza kuwafungua na kutambua mambo muhimu katika makuzi ya mtoto ambayo walikuwa hawayajui awali..

“Nimejifunza unyonyeshaji wa mtoto na jinsi ya kumlinda na malaria, kiukweli kuna changmoto kubwa wanawake wengi wnashauriana kuwapa watoto uji hasa wa udaga kumbe unaweza kumsbaishia matatizo makubwa,” alisema Tatu mkazi wa Igoma.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles