28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Chato yabaki na kijiji kimoja kisichounganishiwa umeme

Veronica Simba – Chato

WAZIRI wa Nishati, Dk. Medard Kalemani, amewasha umeme vijiji vya Rwantaba na Nyarutefye vilivyopo Chato mkoani Geita na kufanya vijiji vilivyofikiwa na nishati hiyo kufikia 114 kati ya 115 vilivyopo kwenye wilaya hiyo.

Akizungumza na wananchi wa Kijiji cha Nyarutefye juzi, muda mfupi kabla ya kuwasha umeme, Dk. Kalemani alisema ifikapo mwisho wa mwezi huu, vijiji vyote vya wilaya hiyo vitakuwa na umeme.

Alisema Chato haitakuwa wilaya ya kwanza kuwashiwa umeme katika vijiji vyake vyote kwani tayari kuna wilaya 34 nchini ambazo hadi sasa vijiji vyake vyote vimefikiwa na huduma ya umeme.

Dk. Kalemani alisema Serikali inaendelea kuunganisha umeme vijijini nchini kote na hadi kufikia Oktoba, vijiji 10,446 kati ya 12,268 vya nchi nzima vitakuwa vimeunganishwa.

“Tutabaki na vijiji 1,822 ambavyo kufikia Juni 2021 vitakuwa vimeunganishwa na kufanya vijiji vyote nchini kuwa vimefikiwa na umeme,” alisema Dk. Kalemani.

Katika hatua nyingine, Dk. Kalemani aliwaasa wananchi ambao umeme umefika katika maeneo yao, kuchangamkia fursa ya kulipia na kutandaza mfumo wa nyaya katika nyumba zao ili waunganishiwe.

Alisema umeme utumike kwa matumizi yenye tija zaidi, hususan kiuchumi badala ya kuutumia kuwasha taa peke yake.

Akijibu hoja za baadhi ya wananchi ambao wamedai kutounganishiwa umeme licha ya kulipia huduma hiyo, Dk. Kalemani aliagiza uongozi wa Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), kuhakikisha wanawaunganishia wote wenye changamoto ya aina hiyo katika kipindi kisichozidi siku 14.

Vilevile, aliwataka watendaji hao wa Tanesco nchi nzima kuharakisha ukarabati wa miundombinu ya umeme iliyoharibika kutokana na mvua zilizokuwa zikinyesha ili kuwaondolea wananchi adha ya ukosefu wa umeme.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya ya Chato, Charles Kabeho, ambaye aliambatana na waziri katika ziara hiyo, alipongeza utendaji kazi wa Serikali kwani ahadi zake zinatekelezwa na wananchi wanashuhudia.

Katika ziara hiyo, Dk. Kalemani pia aliambatana na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Tanesco, Raymond Seya, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Amos Maganga na maofisa wengine waandamizi kutoka wizarani na katika taasisi hizo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles