27.5 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Chalamila aanza na TRA Mwanza, aitaka kutotumia nguvu

Na Sheila Katikula, Mwanza

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Albert Chalamila ameitaka Mamlaka ya mapato Tanzania (TRA) mkoani hapa kukusanya mapato bila kutumia nguvu na badala yake  watumie ubunifu na elimu katika zoezi hilo sanjari na kuwataka wafanyabiashara kujitambua na  kulipa kodi halali bila kusumbuliwa.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Albert Charamila akikamilisha makaboziano ya ofisi na aliyekuwa mkuu wa mkoa huo, John Mongella (Mkuu wa mkoa wa Arusha kwa sasa). Picha na Sheila Katikula, Mwanza.

Hayo aliyasema jana baada ya makabidhiano ya ofisi alipokuwa akizungumza na wafanyabiashara, Viongozi wa dini, Wakuu wa wilaya, Kamati ya ulinzi na usalama, viongozi wa vyama vya siasa mbalimbali na watumishi wa umma.

Amesema ni vyema Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kukusanya kodi halali kwa wafanyabiashara hao ili ziweze kutumika kwenye miradi mikubwa na midogo iliyopo mkoani hapo.

Amesema Rais Samia Suluhu Hassan amesisitiza ukusanyaji wa mapato bila kutumia nguvu kulenga kuongeza hamasa kwa wafanyabiashara nchini kulipa kodi kwa wakati.

Amesema Mkoa wa Mwanza ni kitovu cha biashara anatarajia kukaa na wafanyabiashara ili waweze kuweka mikakati na mbinu za kuhamasisha uwekezaji mkoani hapa sanjari na kuhamasisha wananchi  kufanya kazi kwa  bidii ili kukuza kasi ya maendeleo ya mkoa.

Aidha, amewataka baadhi ya Wazee wenye uwezo kutotumia vibaya msamaha ya matibabu inayotolewa na serikali badala yake kuwaachia ambao hawana uwezo wa kifedha waweze kupata huduma hiyo.

“Serikali imetoa msamaha kwa wazee, watoto na wajawazito watibiwe bure lakini unakuta mtu kapaki gari lake la thamani  anasubiri huduma hiyo kwanini tusiwaachie watu wengine ambao hawana uwezo  wa kulipia matibabu na kununua dawa ili waweze kutibiwa,” ameeleza Chalamila.

Nae, Mkurugenzi wa Uhuru hospitali, Dk. Derick Nyasebwa amewaomba wananchi kuwekeza kwenye  sekta ya afya kwani bila kuwa na afya njema  huwezi kufanya maendeleo yoyote, inasikitisha kuona kuna baadhi ya watu huthamini kununua nguo na kufanya starehe.

“Kuna baadhi ya watu huthamini kununua nguo, kufanya starehe, kununua vijora na hawaoni umuhimu wa kuwekeza fedha zao kwenye matibabu kwa kukata  bima za afya ambazo ni mkombozi pindi unapoumwa na badala yake hutegemea misamaha inayotolewa na serikalini wakati mtu anauwezo wa kujihudumia mwenyewe,” amesema Dk Nyasebwa.

Kwa upande wake Mfanyabiashara wa kampuni ya Birchand Group inayojishughulisha na uuzaji wa mafuta ya kupikia ya pamba na ununuzi wa pamba, Mohamed Ibrahim amesema watahakikisha washirikiana kwa pamoja na Mkuu huyo wa Mkoa kama ilivyokuwa kwa mtangulizi wake John Mongella, ili waweza kulipa kodi kwa wakati na kupelekea mkoa huo kupata maendeleo.

Naye aliyekuwa Mkuu wa Mkoa huo ambaye kwa sasa  amehamishiwa mkoa wa Arusha, John Mongela amewataka wananchi, viongozi wa dini pamoja na watumishi wa sekta mbalimbali kuendelea kushirikiana na kiongozi huo ili waweze kufanya kazi kwa pamoja.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles